Makampuni mbalimbali ikiwa ni pamoja na Facebook na Google nchini Marekani yamepiga marufuku mfanyakazi yeyote kurudi kufanyia kazi ofisini kama hajapata chanjo ya Covid19.
Hatua hii imechukuliwa pia na makampuni mengine kama vile Twitter, Salesforce, na inasemekana hatua kama hii itegemewe kwenye makampuni na mashirika mengine makubwa ya kiteknolojia nchini humo.
Kwa kipindi kirefu tokea janga la Korona lianze makampuni haya na mengine mengi ya nchini humo yameruhusu wafanyakazi wake kufanya kazi wakiwa majumbani. Kampuni kama Twitter imeenda mbali zaidi na ata kufunga baadhi ya ofisi zake moja kwa moja ikipitisha sera ya kufanya kazi kutokea nyumbani kuwa ni ya kudumu, itaruhusu baadhi ya wafanyakazi wake kuendelea kwenda maofisini ila inategemea wengi zaidi kuchagua kufanya kazi kutokea majumbani.
Muhimu vya kufahamu kwa makampuni mbalimbali;
- Apple – Wamesogeza mbele muda wa kuruhusu wafanyakazi kuanza kurudi maofisini hadi mwezi wa Oktoba, utakapofika muda huo wataruhusu wafanyakazi kwenda maofisini angalau mara 3 kwa wiki.
- Microsoft – Wanategemea kufungua ofisi zake kuanzia mwezi Septemba. Msimamo wa kampuni ni kuendeleza sera ya kuruhusu wafanyakazi kufanya kazi majumbani na siku zingine maofisini, ata baada ya janga la korona kuisha kabisa.
- Facebook – Nao wanategemea kufungua ofisi mwezi Oktoba, sera itakuwa kuruhusu baadhi ya wafanyakazi kuendelea kufanya kazi majumbani – ila kwa ruhusa maalumu kama aina ya kazi zao hazina uhitaji sana wa kuwa maofisini.
- Amazon – Kufikia mwisho wa mwaka wafanyakazi wengi waliokuwa wanafanya kazi kutokea majumbani wataanza kwenda maofisini, inategemewa watapata siku mbili kwa wiki za kufanya kazi wakiwa majumbani.
Uamuzi uliochukuliwa na baadhi ya haya makampuni kwa kuweka ni lazima wafanyakazi wawe wamepiga chanjo unaonekana ni uamuzi ambao utakuja kwa baadhi ya makampuni mengi katika mataifa mbalimbali huko mbeleni. Tayari kwa sasa kwa nchini Ufaransa watu ambao hawajapata chanjo wanaweza kukataliwa kuingia kwenye migahawa au sehemu zingine zenye watu wengi, ikiwa ni hatua ya kusaidia kuwakinga wengine dhidi ya maambukizi ya kovidi.
Je una mtazamo gani juu ya uamuzi huu?
Chanzo: NPR
No Comment! Be the first one.