Kwa miaka kadhaa sasa kama unakuwa hufanyi mawasiliano kupitia WhatsApp unaweza ukaonekana wa kushangaza kwa wengi kutokana na programu tumishi ilivyotokea kupata watumiaji wengi zaidi duniani hivyo basi kurahisisha mawasiliano ambayo uti wa mgongo ni intaneti!
Inawezekana kabisa umeacha kutumia dakika nyingi za kuongea na simu badala yake sasa unanunua kifurushi cha intaneti ambacho kitakutosheleza kulingana na mahitaji yako hivyo basi kuweza kupiga simu kwa njia ya sauti/picha jongefu.
WhatsApp inaendelea kuifanya iendelee kuwavutia watu kwa kuwaunganisha watumiaji wengi kwa wakati mmoja; kama umeshawahi kufanya mawasiliano na mtu zaidi ya mmoja kwenye programu tumishi husika iwe kwa njia ya picha mnato au sauti basi utakubaliana na mimi huwezi kuunganisha watu zaidi ya watatu (3) nyote mkajumuika kwenye mazungumzo pamoja.
Nikufahamishe tuu kuwa maboresho yapo njiani ambapo watu zaidi ya wanne au zaidi wataweza kuwasiliana kupitia WhatsApp wote kwa wakati mmoja. Hatua hiyo inafuatia baada ya washindani wenza kama Google kuboresha Google Duo kwa kuruhusu watu wengi zaidi kuweza kuwasiliana kwa pamoja.
Maboresho hayo yameaanza kuonekana kwa watu wachache wanaotumia WhatsApp Beta hivyo basi sisi wengine tusubiri mpaka hapo sasisho hilo litakaporuhusiwa kupatikana kwa wengineo. Vipi unafikiri hatua hii itawavutia watumiaji wengi kutumia picha jongefu kuwasiliana?
Vyanzo: GSMArena, First Post