Fahamu Intel waitetea Huawei dhidi ya katazo la kibiashara la serikali ya Marekani. Nje ya Google ni makampuni mengi sana mengine ambayo yameathirika na katazo la kujihusisha na Huawei kibiashara.
Ingawa kwenye biashara ya simu tayari inaonekana Huawei ataweza kufanikiwa kiasi flani kuendelea kutengeneza simu kwa kutumia toleo lao spesheli la Android ila kwenye biashara ya utengenezaji laptop ambapo tayari walianza kupata sifa za ubora na ubunifu ndio biashara ambayo imeathirika zaidi.
Kumbuka kutokana na katazo hili hawataweza ata kupata toleo la programu endeshaji la Windows kutoka Microsoft, na pia ata baadhi ya vipuli muhimu vinavyotumika kama vile kutoka Intel pia hawataweza kuvipata.
Kampuni ya Intel imesema inafanya kazi kubwa ya ziada kuweza kufanikisha katazo la kibiashara dhidi ya Huawei kuondolewa na serikali ya Marekani. Ingawa Huawei inawakilisha asilimia 1 tuu ya mapato ya Intel ila soko la China linawakilisha zaidi ya robo ya mapato ya kampuni ya Intel kwa mwaka 2018 – ambapo mapato yalikuwa dola bilioni 70.8 za Marekani (Takribani Tsh Trilioni 162.74).
Intel wamesema hali ya sasa haina faida kiusalama. Suala ambalo wapo tayari kushirikiana na serikali ya Marekani kufanya ni kuhakikisha wanapitia vizuri teknolojia ya Huawei na kuihukuma kwa matokeo ya kweli na si kwa kutaka kuharibu biashara nzima bila kuwa na ushahidi – kwani wanaoathirika ni wengi zaidi ya Huawei tuu.
Hii ni orodha ya baadhi ya makampuni makubwa ambayo kwa sasa imewabidi kuvunja uhusiano wa kibiashara na Huawei;
- Google: Google ndio maarufu zaidi kwa kuwa ndio inawakilisha eneo la biashara ambalo tayari Huawei ilianza kufanya vizuri sana. Nalo ni eneo la simu janja. Google inawabidi kuvunja uhusiano wa kibiashara wa kuwapatia Huawei toleo lao la Android linalokuja na Google PlayStore na apps mbalimbali za Google.
- Facebook: Facebook tayari wametoa taarifa kwa Huawei kuwataka wasiweke apps za Instagram, Facebook, Messenger, WhatsApp au apps nyingine zozote zinazotengenezwa nao. Simu zinazotoka kwenye viwanda vya Huawei kwa sasa hazitakuja na apps hizi
- Intel: Kama tulivyoelezea hapo juu, Intel ni kampuni maarufu kwa ajili ya vipuli hasa hasa vya kompyuta. Wao pia hawatakiwi kufanya biashara na Huawei
- Microsoft: Katazo hili lina maanisha kama Huawei anataka kutengeneza kompyuta basi itambidi alete kompyuta zinazokuja na programu endeshaji za Linux. Lakini pia ni vigumu kutengeneza kompyuta zenye ubora bila kutumia vipuli muhimu kutoka Intel. Kwa kifupi biashara ya kompyuta imeharibika vibaya sana.
- Qualcomm Inc, Xilinx Inc na Broadcom Inc ni makampuni mengine muhimu kwenye teknolojia za vipuli kwa ajili ya mawasiliano – teknolojia zake zinatumika kwenye kompyuta na kwenye simu. Hawa pia wameshasema hawawezi kufanya kazi na Huawei kwa sasa.
- Qorvo Inc: Ni kampuni ya teknolojia za mawasiliano ya mfumo wa redio. Kampuni hii ya Marekani nayo imesema inategemea mapato yako ya asilimia 15 kupotea – hii ikiwa ni dola milioni 50 za Marekani (yaani wanapoteza mapato ya takribani Tsh Bilioni 114).
- ARM: ARM ni kampuni maarufu ya utengenezaji wa vipuli vya teknolojia za mawasiliano za mfumo wa ‘chips’. Ingawa kampuni hii ni ya Uiengereza, inamilikiwa na benki ya Japan ya SoftBank Group na wao wamesema watafuata sheria ya Marekani na hivyo wamevunja uhusiano na Huawei kwa sasa.
- Panasonic: Kampuni ya Kijapani ya Panasonic imesema kuanzia Mei 21 iliacha mara moja kuiuzia Huawei baadhi ya vipuli ambavyo vina baadhi ya teknolojia ya Marekani.
Kwa kifupi suala hili litawaathiri Huawei vikubwa tuu, ila pia makampuni mengi ya Marekani nayo yataumia vibaya kimapato na ndio maana tumeshaona juhudi za Intel na Google za kuhimiza serikali ya Marekani kubadili uamuzi wake.
Watafiti wengi wa masuala ya kisiasa na kibiashara wanaamini katazo hili ni sehemu ya vita ya kiuchumi ya chini chini kati ya Marekani na Uchina. Serikali ya Trump ikijaribu kuzuia ukuaji wa kasi wa kiuchumi na kiteknolojia wa taifa la Uchina.