Apple wanaleta simu mpya za iPhone kila mwaka, ila kwa mwaka huu kupitia iPhone SE mpya wanaonesha ni kwa namna gani wana lengo la kuleta simu ya iPhone itakayoshindana na simu za bei ya kati kutoka Samsung, Google, Huawei na wengine.
Leo tunakuonesha ni kwa nini simu hii ya iPhone SE ni moja ya toleo lililo la kiwango cha juu ukilinganisha na bei yake na pia ni kwa nini litakuwa tishio kwa simu zingine za Andrid.
Bei: $399 (Tsh 925,000 – Tsh 1,000,000/= kwa toleo la GB 64)
Bei yake ni moja ya sababu. Kwa takribani milioni 1 kwa bei ya nje, tukitegemea haitozidi Tsh milioni 1.2 – 1.4 kwa Tanzania hii inamaanisha iPhone SE ni moja ya simu ya bei nafuu zaidi kutoka Apple katika miaka hii miwili.
Prosesa: A13 Bionic – prosesa ile ile kama kwenye iPhone 11 Pro
Simu hii inakuja na moja ya prosesa yenye ufanisi mkubwa kwenye simu janja kwa sasa, hii ni prosesa inayotengenezwa na Apple wenyewe, prosesa inayokuja kwenye simu yao ya hadhi ya juu ya iPhone 11 Pro. Prosesa hiyo hiyo imetumika kwenye toleo hili la iPhone SE. Nje ya faida ya ufanisi wa simu pia ina maanisha simu hii itapata masasisho ya kisasa ya programu endeshaji ya iOS kwa miaka minne au zaidi kuanzia mwaka huu. Huu ni muda mrefu na wa uhakika, simu nyingi upande wa Samsung na Android kwa ujumla mara nyingi zinapata masasisho ya programu endeshaji ya kisasa kwa muda wa miaka miwili hadi mitatu tuu.
Betri: Kiwango sawa na iPhone 8
iPhone SE hii haimaanishi unapunguziwa uwezo, kama vile kwenye prosesa, kwenye betri pia haijanyimwa. Inakuja na kiwango sawa cha betri na iPhone 8. Kwa iPhone SE betri hili linaonesha litadumu muda mrefu ukichaji kwani ukubwa wa display/kioo ni mdogo ukilinganisha na iPhone 8.
Kamera ya kisasa na yenye ubora: Megapixel 12 kamera kuu na megapixel 7 kwa kamera ya selfi.
Kwenye kamera kuna utumiaji wa teknolojia ya kisasa kuhakikisha picha zinaboreswa vizuri na programu endeshaji (OS/AI). Kwa walioweza kupata simu hii mwanzoni kabisa kwa majaribio wameonesha hakuna tofauti kubwa sana utaiona katika picha za simu hii na picha za iPhone 11 Pro ( Simu inayopatikana kwa takribani zaidi ya Tsh milioni 3).
Ubora wa picha zake unasaidiwa pia na utumiaji wa prosesa ya kisasa ya A13 Bionic. Kamera yake pia ina uwezo wa kurekodi video za 4K/60fps. Hichi ni moja ya kiwango cha juu kabisa cha ubora wa video.
Mengineyo…
Sifa zingine za kitofauti kwa bei yake ni pamoja na kuja na teknolojia ya kuchaji bila kuunganisha na waya (wireless charging), pia kuweza kuweza kutolowa kwa urahisi na kingine ni kuweza kutumia vivalisho (cases) vya simu ya iPhone 8 – hakuna tofauti ya ukubwa na simu hiyo. Je wewe unaweza kuishi na simu isiyo na sehemu ya kuchomeka waya wa earphone? Yaani kutumia earphone zinazotumia mfumo wa bluetooth, kwani iPhone hii haiji na tundu hilo.