Je unataka maisha yako baada ya kifo yaweje? Microsoft wamechukua hatua ambazo zinaonesha wanataka watu wakifa waendelee kuwa hai kupitia mifumo ya akili bandia ya kompyuta, yaani AI. Ndugu au wanafamilia wako waweze kuchati na wewe.
Je ni jambo linalowezekana?
Kwa muda mrefu bado sayansi na teknolojia inatumika katika kutafuta jinsi ya kuongeza maisha ya binadamu duniani, iwe kupitia matibabu ya afya au kupitia teknolojia nyingine ngumu, mfano kama ile ya kuwezesha upasuaji wa kuhamisha kichwa cha mtu aliyehai na kukipachika kwenye mwili mwingine – Soma kwa kubofya hapa. Inaonekana wanateknolojia bado wanatafuta kila namna ya kuhakikisha wakishinde kifo – yaani ata kama sio kukishinda kabisa, basi kinamna flani tuu.
Microsoft wamelipia hakimiliki ya ubunifu wa mfumo wa teknolojia unaokusanya data za mitandao ya kijamii ya mtu, yaani jinsi mtu huyu anazungumza/kupost mambo kwenye mitandao ya kijamii na huwa anajibu vipi maongozi. Kupitia teknolojia wanayobuni wanataka pia watu wawe na uwezo wa kuipa huduma hiyo rekodi ya sauti zao na matamshi ili kuwezesha utengenezwaji wa nafsi ya kidigitali, inayotegemea akili bandia ya kompyuta, yaani AI.
Kwa kutumia maelfu ya data za mitandao yako ya kijamii wanataka huduma hii iweze kutengeneza nafsi kama yako, na kuweza kuzungumza au kujibu maswali kama vile ambavyo wewe ungeweza kujibu.
Microsoft wanategemea huduma hiyo kuwapa nafasi watu ambao ata bado wako hai kuweza kuchati na nafsi zao kidigitali, na kupata nafasi ya kuzifundisha majibu sahihi ya maswali au mazungumzo watakayokuwa wanauliza n.k. Bot / ‘roboti’ ambaye anatakiwa awe anawasiliana kama wewe, atakuwa na uwezo wa kutumia maandishi kupitia chati, au kutuma picha na video.
Itatokea nini utakapoaga dunia?
Lengo kuu ni kuwapa nafasi watu unaowapenda kuweza kuwa na uwezo wa kuja kwenye huduma hii na kuchati na wewe tena. Ingawa kwa sasa watakuwa wanawasiliana na nafsi yako ambayo imetengenezwa na mfumo wa teknolojia ya AI/Akili bandia ya kompyuta, kulingana na jinsi inavyokufahamu kupitia data zako za mitandao ya kijamii na kile ambacho umekifundisha wewe.
Kwa sasa kuna suala kubwa kuhusu usalama wa data za watumiaji wanaotumia huduma za kimitandano kama WhatsApp na ata Facebook na mingine mingi, Microsoft nje ya kumiliki LinkedIn na Skype, hana umiliki wa mitandao mikubwa ya kijamii – hivyo inaonakata watakapotaka kuanzisha huduma hiyo basi lazima mtumiaji wa mtandao wa kijamii akubali kujitengenea mwenyewe nafsi yake hii ya kidigitali.
Je una mtazamo gani kuhusu ubunifu wa huduma hii? Kwa sasa Microsoft wamechukulia hakimiliki ya ubunifu wa huduma hii, bado hawajaanza matengenezo. Na kumbuka si kila huduma au teknolojia inayolipiwa hakimiliki huja kipindi hichohicho.
Vyanzo: Forbes na vyanzo mbalimbali
No Comment! Be the first one.