Uwepo wa majukwaa ya kujifunzia mtandaoni umetengeneza urahisi kwa watu kupata ujuzi mbalimbali, kujifunza na kupata cheti mtandaoni. Unapoperuzi mtandaoni unapata nafasi ya kujifunza mengi na kujiongezea ujuzi utakaokusaidia katika biashara au taaluma yako.
Katika majukwaa haya ya kujifunzia mtandaoni kuna baadhi ya kozi ni za bure na zingine ni za kulipia. Pia kuna baadhi ya majukwaa yameingia ubia na vyuo duniani na kutoa shahada za masomo kwa kusomea mtandaoni. Majukwaa haya ya kujifunzia mtandaoni yanakuhitaji uwe umetengeneza akaunti ili uweze kutumia huduma zao.
Yafuatayo ni baadhi ya majukwaa unayoweza kutumia kujifunza mtandaoni:
Udemy
Hili ni jukwaa linalotoa nafasi kwa mtaalamu kuuza ujuzi wake mtandaoni kwa kuandaa video pamoja na nyenzo mbalimbali zitakazoelezea vizuri mada anazofundisha ili kumrahisishia huduma mtu anayejifunza. Unaweza kutengeneza akaunti katika jukwaa hili kama mwanafunzi unayetaka kujifunza au kama mwalimu anayetaka kufundisha na kulipwa mtandaoni. Pia jukwaa hili linatoa baadhi ya kozi bure kulingana na uamuzi wa mtaalamu anayefundisha kama ataruhusu kozi yake kutolewa bure au kutaka malipo. Kuna zaidi ya kozi 155,000 zinazofundishwa katika jukwaa hili.
Coursera
Jukwaa hili linatoa nafasi kwa vyuo na makampuni mbalimbali duniani kuuza kozi wanazofundisha mtandaoni. Kwa kupitia jukwaa hili mwanafunzi anaweza kujisajili na kusomea shahada anayotaka kupitia chuo atakachokichagua. Kozi zote zinazopatikana katika jukwaa hili ni za kulipia ingawa wanatoa siku saba za kwanza bure kwa watumiaji wapya. Jukwaa hili linashirikiana na zaidi ya vyuo na makampuni 200 kutoka katika nchi tofauti tofauti. Baadhi ya vyuo na makampuni yaliyopo katika jukwaa hili ni kama Google, IBM, Stanford na Imperial College London.
edX
Hili ni jukwaa la kujifunzia mtandaoni lenye zaidi ya kozi 3000 kutoka katika vyuo vikuu mbalimbali duniani zaidi ya 160. Katika jukwaa hili utachagua kozi unayotaka kusoma au utaperuzi katika chuo unachotaka kusomea na kuangalia ni kozi ipi wanayotoa inayokufaa. Kozi zote katika jukwaa hili ni za kulipia lakini malipo yanafanyika kulingana na kozi husika, kila kozi ina bei yake ya kulipia. Kwasababu kozi hizi zinatolewa na vyuo vinavyotambulika duniani unapokamilisha masomo unapewa na cheti kabisa cha shahada uliyosomea. Baadhi ya vyuo vinavyofundisha kupitia jukwaa hili ni Boston University, Harvard University na Australian National University.
Google Digital Skills for Africa
Kampuni ya Google imetengeneza jukwaa maalum kwa ajili ya watu waliopo Africa kujifunza kozi mbalimbali zinazohusu matumizi ya mtandao. Kwa kushirikiana na makampuni na vyuo vikuu zaidi ya 15 Google wameweza kuandaa kozi 156 zinazohusu matumizi ya mtandao, usalama wa mtandao, kusajili biashara yako mtandaoni na mada zingine nyingi zinazolenga kusaidia watu kutumia huduma za mtandaoni zaidi katika shughuli zao. Katika kozi hizo kuna ambazo zinatolewa bure na zingine ni za kulipia. Kwa zile kozi zinazotelewa moja kwa moja na Google wenyewe zote ni za bure lakini zile kozi zinazotolewa na vyuo shirikishi ndio za kulipia.
No Comment! Be the first one.