Mtandao ni muunganiko na muingiliano wa mawasiliano baina ya kompyuta mbalimbali duniani zinazo badilishana taarifa. Katika chanzo cha mtandao ruta zinazotumika huwa ni nyingi na zenye uwezo mkubwa wa kusambaza taarifa kwa haraka.
Ruta ni kifaa maalum kinachotumika kusambaza taarifa za mtandaoni kupitia nyaya za fiber optic zinazo unganisha ruta moja na nyingine.
Vyanzo hivi vya mtandao husimamiwa na kumilikiwa na Kampuni za kibiashara, Serikali na Mashirika ya kielimu. Vyanzo vya mtandao vimegawanyika katika makundi matatu ambayo ni Tier 1, Tier 2 na Tier 3. Tier 1 ndio chanzo kikuu cha mtandao ambacho kinakuwa na washiriki wachache wanaoweza kushirikiana miundombinu ya usambazaji wa mtandao bila kulipishana kwani wanaingiza faida ya kutosha kwa huduma wanayotoa. Baadhi ya makampuni yaliyo katika kundi hili ni AT&T, CenturyLink, Sprint na Global Telecom and Technology (GTT).
Tier 2 na Tier 3 huwa ni washiriki wa kusambaza huduma za mtandao wanaolipia kuunganisha ruta zao katika mkondo wa fiber optic unaotoka moja kwa moja kwa Tier 1. Tier 2 mara nyingi huwa ni Serikali au Makampuni makubwa ya Mawasiliano yenye miundombinu ya kusimamia usambazaji wa mtandao katika nchi yake na nchi jirani. Tier 3 huwa ni makampuni ya Mawasiliano yanayotoa huduma mbalimbali za mtandao kwa kununua huduma za usambazaji wa mtandao kwa Tier 1 au Tier 2 na kuuzia mteja rejareja.
Katika usambazaji wa mtandao makampuni husika hujitahidi kuwa na chanzo zaidi ya kimoja cha mtandao ili wasishindwe kutoa huduma kwa wateja wao linapotokea tatizo la kiufundi. Ushirikiano huu hutokea hadi kwa washiriki wa vyanzo vikuu vya usambazaji wa mtandao (Tier 1) ambao hushirikiana wao kwa wao bila kulipishana. Ruta zinazotumika katika usambazaji wa mtandao kwa vyanzo vikuu huwa na kasi kubwa inayofika hadi gigabiti 100 kwa sekunde (100GBps) na hutengenezwa na makampuni makubwa ya teknolojia ya mitandao kama Cisco, Huawei na Extreme.
Tanzania ni moja kati ya nchi iliyobahatika kupokea Mkondo wa fibre optic uliopitia baharini na kuwezesha usambazaji wa mtandao nchini na nchi jirani. Mkondo huo wa fibre optic hutokana na vyanzo mbalimbali kama 2Africa, Eastern Africa Submarine System (EASSy), SEACOM/Tata TGN-Eurasia na Seychelles to East Africa System (SEAS).
No Comment! Be the first one.