Gazeti mashuhuri la nchini Marekani, Wall Street Journal katika uchunguzi wao wamebaini wafanyakazi wa Huawei wanahusika na udukuzi na kusaidia shughuli za kijasusi dhidi ya wanasiasa barani Afrika.
Katika uchunguzi wao wamesema wamepata uhakika zaidi hasa kwenye mataifa kama Uganda na Zambia. Wamesema uchunguzi wao haujapata uhakika kama viongozi wa juu wa kampuni hiyo makao makuu wanafahamu kuhusu yale yanayofanywa na wafanyakazi wao katika nchi hizo.
Shutuma za gazeti hilo zinasema wafanyakazi wa Huawei wamekuwa wakitoa msaada wa serikali kufuatilia mawasiliano ya wapinzani wao kisiasa kupitia teknolojia za mawasiliano ya simu, hii ikiwa ni pamoja na kutuma taarifa za walipo, na kurekodi mawasiliano yao ya njia ya simu na mitandao ya kijamii.
Inasemekana kwa Uganda wafanyakazi wa kampuni hiyo walitoa msaada kwa vitengo vya kiusalama kuweza kufungua na kusoma meseji za kwenye simu ya mwanamuziki na mwanasiasa Bobi Wine.
Wafanyakazi hao walifanikisha hayo kwenye ofisi za makao makuu ya jeshi la polisi la nchini humo, walitumia programu ya udukuzi inayofanana kiutendaji na programu maarufu ya kampuni moja ya Israel, NSO Group, inayokwenda kwa jina la Pegasus spyware.