Google wanakuja na teknolojia ya Fastshare ambayo itapatikana katika toleo lijalo la Android ambalo linaenda kwa jina la Android Q kwa sasa – jina kamili hutambulishwa mbeleni.
Mtumiaji wa Android wataweza kutuma na kupokea mafaili makubwa kutoka kwa mtumiaji mwingine kwa kasi zaidi.
Kwa muda mrefu kwenye Android teknolojia ya kuhamisha mafaili kutoka simu moja hadi nyingine imekuwa ni teknolojia ya Android Beam. Teknolojia ya Android Beam imekuwa ikitegemea kifaa cha teknolojia ya NFC – ambayo ilikuwa inawezesha kutuma mafaili kutoka simu moja hadi nyingine ila kwa KASI NDOGO.
Teknolojia mpya ya Fastshare itakuja ikiwa inategemea teknolojia ya Bluetooth pamoja na teknolojia ya WiFi ambayo ipo kwenye simu janja zote kwa sasa. Kwa kutumia teknolojia ya WiFi mafaili yataweza kutumwa kwa kasi zaidi.
Kwa muda mrefu tayari Apple alileta teknolojia ya namna hii kwa vifaa vyake vya iOS na MacOS – ikitambulika kwa jina la AirDrop. Mtumiaji mmoja wa kifaa cha Apple anaweza kutuma faili kubwa kwenda kifaa kingine ndani ya sekunde hadi dakika chache.
Inavyofanya kazi;
- Kwa kutumia teknolojia ya Bluetooth – vifaa viwili vinatengeneza mawasiliano na kuandaa teknolojia ya WiFi kutumika
Kisha kwa kutumia teknolojia ya WiFi mafaili yanatumwa kutoka kifaa kimoja kwenda kingine - Kumbuka haitumii huduma ya intaneti ya kawaida, haya ni mawasiliano ya moja kwa moja kutoka kifaa kimoja kwenye kingine.
Uzuri wa FastShare kutoka Android ni kwamba watumiaji wataweza kutuma mafaili hadi kwa vifaa vya Apple, wakati kwa AirDrop mawasiliano ni kati ya vifaa vya Apple tuu.