Digital footprint ni alama ya kidigitali ambayo huachwa na mtu anapomaliza kutumia mtandao. Alama hii hubeba kumbukumbu za mambo uliyoyafanya wakati unapokuwa mtandaoni.
Digital Footprint inaweza husisha historia yako ya matendo yako mbalimbali, kama vile uandikaji wako wa maoni yako kwenye mitandao wa kijamii, kutuma picha au video katika mitandao ya kijamii pamoja na kuchapisha andiko kwenye tovuti yako mtandaoni.
Kutokana na taarifa nyingi za watu kuwa mtandaoni siku hizi imekuwa ni rahisi sana mtu anayejua majina yako kukutafuta na kuona taarifa zaidi kuhusu wewe zilizopo mtandaoni. Kwa hali hii inabidi uwe makini sana na mambo unayoyafanya wakati unatumia huduma yeyote ile mtandaoni.
Waajiri wa siku hizi wamekuwa wakiitumia sana njia hii kufahamu zaidi kuhusu tabia na mienendo mbalimbali ya mtu kabla hawajamuajiri. Ni vigumu mno kufuta taarifa zako zilizopo mtandaoni unaweza ukajaribu na kufanikiwa lakini kuna ambazo bado zitabaki cha kuzingatia ni kuhakikisha kuwa unakuwa makini katika mambo unayojihusisha nayo unapokuwa mtandaoni.
Unaweza kutumia njia zifuatazo kuchunguza na kutengeneza kumbukumbu nzuri mtandaoni.
- Jitafute Google: Hatua ya kwanza ni kulitafuta jina lako Google ili uweze kuona na kufahamu kumbukumbu yako iliyotunzwa au inayoonekana sana mtandaoni. Ukifanya hivi utaweza kuona ni wapi ambapo una rekodi mbaya na kuanza mchakato wa kufuta kumbukumbu hiyo kama inawezekana. Pia kwa kufanya hivi utajua ni mtandao gani wa kijamii ambao unavujisha baadhi ya taarifa zako binafsi ili uweze kwenda na kurekebisha kitu hicho kwa kuongeza ulinzi kwenye akaunti yako, kufuta akaunti yako au kufuta taarifa zako binafsi ulizozijaza huko.
- Linda taarifa zako: Hakikisha kuwa unazilinda taarifa zako zote binafsi ulizozijaza kwenye mitandao ya kijamii au kwenye baadhi ya tovuti. Njia nzuri ya kufanya hivi ni kwa kuziongezea ulinzi ambapo kuna baadhi ya mitandao ya kijamii inaruhusu mtu kuficha taarifa zake binafsi.
- Fikiria kabla haujatuma kitu mtandaoni: Unapotaka kuandika maoni yako mtandaoni au kutuma picha na video unatakiwa kwanza kujiuliza mara mbilimbili athari za kutuma hicho kitu maana utakuwa umejitengenezea kumbukumbu mbaya au nzuri mtandaoni.
- Futa akaunti zote usizozitumia: Katika matumizi yako ya mtandao unaweza ukawa umejisajili katika baadhi ya huduma za mtandaoni zinazotolewa katika tovuti mbalimbali kama umeshamalizana na huduma zao au kama hauzihitaji tena huduma zao ni vyema ukajifuta usajili huko ili waache kukutumia barua pepe zao pamoja na kufuta akaunti yako ili wasiwe na taarifa zako tena.
No Comment! Be the first one.