Kama bado unatumia simu ya iPhone 5 itakubidi uchukue hatua ya kusasisha(update) OS – programu endeshaji ili kuepuka matatizo.
Kuna maboresho ya teknolojia ya GPS – teknolojia inayotambua eneo/mahali kilipo cha elektroniki kwenye mfumo wa ramani ya dunia. Teknolojia ya GPS inatumika pia kuhakikisha simu yako inatoa taarifa sahihi hasa hasa kwenye suala la muda – na kuna apps nyingi zinazotumia huduma ya intaneti ambazo zitashindwa kufanya kazi vizuri kama mipangilio ya GPS ina matatizo.
Apple wameanza kutuma taarifa kwa watumiaji wa iPhone 5 na kuwataka kusasisha toleo la iOS kwenye sasisho la kisasa zaidi linalopatikana eneo la mipangilio/settings.
Kama hautasasisha huduma ambazo zinaweza zisifanye kazi vizuri ni pamoja na;
- Barua pepe – email
- Kivinjari (browser)
- Soko la App Store
- Huduma ya iCloud
Kwa mtumiaji wa iPhone 5 unatakiwa kuhakikisha simu yako inatumia toleo la iOS 10.3.4 – ndio toleo la kisasa zaidi kwa simu hizo. Kama ikifika Novemba 3 na mtu utakuwa bado haujasasisha njia pekee ya kufanya hivyo itakuwa ni kwa kutumia kompyuta – na itafuta simu nzima, na hivyo utatakiwa ufanye ‘backup’ kabla.
Ingawa watumiaji wengi wa iPhone tayari wanatumia za kisasa ila bado kuna kundi dogo la watumiaji bado wanatumia matoleo ya nyuma ya iOS na ndani yake wapo wa iPhone 5.
Vyanzo: Apple