Huawei na 6G. Wakati ata bado 5G haijaanza kusambaa sana tayari kampuni ya Huawei imeanza utafiti wa teknolojia ya 6G.
Kampuni ya Huawei tayari imezipiku kampuni nyingi duniani katika uwekezaji na utengenezaji wa teknolojia na vifaa vya mawasiliano vya 5G vyenye ufanisi mzuri na pia kwa bei nafuu kuliko makampuni mengine mengi duniani.
Watafiti wengi wanaamini itachukua zaidi ya miaka miwili teknolojia ya 5G kusambaa na kutumika sehemu nyingi duniani kote, lakini hilo haliwafanya Huawei wasimame. Huawei hawataki kulala na inasemekana tayari wameanza utafiti wa kuja na teknolojia ya 6G umeanza kupitia kitengo chao cha utafiti (R&D) kilichopo jijini Ottawa nchini Kanada.
Kwa makadirio ya haraka teknolojia hiyo itaanza kupatikana kwenye miaka ya 2030.
Mafanikio ya Huawei kwenye teknolojia ya 5G yameipa Marekani wakati mgumu kwani makampuni ya nchini humo na pamoja ya mataifa mengine ya magharibi bado hayajafikia kiwango cha ubora na unafuu wa teknolojia na bidhaa za 5G ukilinganisha na Huawei. Huawei kuwa kampuni ya kutoka nchini China linawapa wakati mgumu na hivi karibuni kumekuwa na jitihada kadhaa zinazoonesha harakati za Marekani kujaribu kufanya mataifa rafiki kutonunua vifaa vya teknolojia ya 5G kutoka Huawei.