Mpango wa Facebook wa kuja na sarafu ya kidigitali inayobeba jina la Libra bado unapambana na serikali ya Marekani na za mataifa mengine yenye nguvu kabla ya kuweza kufahamu kama utafanikiwa au vipi.
Mkurugenzi Mkuu wa Facebook, Bwana Mark Zuckerberg anatakiwa kukutana na wabunge wa Marekani mwezi huu tena ili kutoa maelezo zaidi kuhusu sarafu ya Libra, mipango yao kuhakikisha usalama na pia kujibu maswali mbalimbali.
Kamati ya huduma za fedha (House Financial Services Committee) imesema Bwana Zuckerberg atakuwa shahidi pekee katika kikao kitakachofanyika tarehe 23 mwezi huu ambacho kitalenga zaidi kuhusu nafasi ya Facebook katika masuala ya fedha.
Mwezi Juni mwaka huu ndio mara ya kwanza Facebook waliweka wazi mipango yao ya kuja na sarafu ya kidigitali, yaani cryptocurrency itakayobeba jina la Libra. Sarafu hiyo itahifadhiwa katika mfumo wa uhifadhi fedha za kidigitali (digital wallet) walioupa jina la calibra. Kupitia Calibra watu wataweza kulipia bidhaa mitandaoni na pia kutuma pesa duniani kote kwa urahisi kwenda kwa watumiaji wengine wa calibra.
Tokea mpango huo uwekwe wazi kumekuwa na malalamiko na hofu kutoka kwa wadau mbalimbali wa fedha – hasahasa serikali mbalimbali. Kumekuwa na ukuaji na umaarufu mkubwa wa fedha za kidigitali tokea ujio wa Bitcoin.
Wakati huko Marekani kikao hichi kinakuja kule Uingereza tayari Benki Kuu tayari imesema itaruhusu sarafu hiyo kama Facebook watafuata taratibu na sheria zote za kibenki kama zile zinazofuatwa na mabenki mengine nchini humo. Suala hili linaweza kuiweka sarafu hiyo kwenye nafasi mbaya ukilinganisha na sarafu zingine za kidigitali.
Pia serikali ya Ufaransa imesema itahakikisha inafanya mazungumzo na serikali zingine katika Umoja wa Ulaya kuhakikisha sarafu hiyo hairuhusiwi kwenye nchi za Umoja huo.
Hali hii ya kisiasa imefanya baadhi ya washirika wa Facebook katika uletaji wa teknolojia na sarafi ya Libra kuanza kuwa na wasiwasi juu ya mafanikio ya sarafu hiyo. Kulikuwa na kundi la wadau 28 kwenye ushirikiano walioupa jina la Libra Association, kampuni ya PayPal inayotoa huduma za malipo ilikuwa moja ya wadau na sasa wamejitoa kwenye umoja huo.
Soma Pia: PayPal ni nini? Ifahamu njia salama ya malipo ya kwa njia ya mtandao