Ugonjwa wa Coronavirus ni ugonjwa ambao umeshika kurasa za mbele za vyombo mbalimbali duniani kote tokea mwanzo wa mwaka. Je makampuni ya teknolojia yameathirika kwa kiasi gani?
Fahamu: Apple wamefunga zaidi ya maduka 50 nchini China kutokana mlipuko wa Coronavirus
Ugonjwa huu tayari umeshaathiri sekta mbalimbali za uchumi duniani kote – hii ikiwa ni pamoja na sekta ya usafiri (kwa safari za kwenda China, na baadhi ya mataifa yaliyoathirika hadi sasa), sekta ya utalii, elimu na biashara.
Je kwenye sekta ya teknolojia wakina nani wameathirika zaidi?
Makampuni makubwa ya teknolojia kama vile Apple, Amazon, Facebook, Aliexpress na mengine mengi yameshakubali kuathirika kwa namna flani kutokana na mlipuko wa ugonjwa huu.
Amazon
- Kampuni kubwa ya mauzo kwa njia za mtandao. Imejikuta ikilazimika kununua na kuhifadhi bidhaa mbalimbali muhimu kutoka China ili kuepuka shida/tatizo ikitokea wakishindwa kupata bidhaa hizo kutoka China. Inakadiriwa asilimia 40 ya wauzaji katika tovuti ya Amazon wanatokea nchini China, na pia asilimia kubwa ya wauzaji wanaoishi nchini Marekani huwa wananunua bidhaa zao kutoka viwanda vya nchini China.
Apple
- Apple wanategemea upungufu wa mauzo ya simu zao nchini China. China imekuwa ni moja ya soko muhimu sana la simu kwa China nje ya Marekani.
- Kipindi cha sikukuu za mwaka mpya wa China huwa ni kipindi cha mauzo makubwa nchini humo, sikukuu hii mwaka hii ilikuwa katika kipindi ambacho ugonjwa huo ulikuwa tayari umelipuka na hivyo kufanya watu wengi kutojitokeza madukani na ata wenye maduka nchini humo sehemu nyingi kufunga biashara zao.
- Pia Apple wamesema kutakuwa na upungufu wa simu zao kwenye mataifa mengine kutokana na kuathirika kwa shughuli za viwanda nchini China.
Biashara ya vipuli vya vifaa vya elektroniki
- Mamilioni ya wafanyakazi katika viwanda vya utengenezaji wa vipuli na bidhaa za elektroniki kama vile simu, kompyuta na magemu waliathirika. Kwa waliokuwa likizo kwa ajili ya mwaka mpya wa China walijikuta wameshindwa kurudi katika miji yao ya kazi baada ya zuio la kusafiri. Suala hili liliathiri ufanyaji kazi wa viwanda vingi nchini humo.
Je kuna waliofaidika?
Huduma za intaneti: Tovuti ya utafiti wa data ya QuestMobile inasema wastani wa muda unaotumika kwenye mtandao nchini China kwa mtu mmoja mmoja umepanda kutoka wastani wa masaa 6.1 kwa siku mwezi Januari hadi kufikia masaa 7.3 kwa siku katika kipindi hichi. Hii ni kwa sababu bado ofisi na shule nyingi zimefungwa.
Apps za Kusoma au Kufanya kazi kwa njia za mtandao
Makampuni ya kiteknolojia yanayotoa huduma za kusoma kwa njia ya mtandao au kuwaleta pamoja wafanyakazi wa kampuni moja kwa njia ya mtandao ndiyo yaliyonufaika zaidi katika kipindi hichi.
- Shule na vyuo vingi vya nchini China zimejikuta zikilazimika kuendelea kutoa huduma za elimu kwa wanafunzi wake kwa njia za mtandao.
- Pia wafanyakazi wanaoendelea kufanya kazi zisizo za ulazima wa kukutana – hasa hasa maofisini, wamejikuta wakitumia huduma za kisasa za kuchati na kuweza kutumiana mafaili kwa urahisi kwa njia za mtandao. Makampuni kama DingTalk(ya Alibaba), Lark na WeChat Work ya nchini humo yamepata ukuaji wa asilimia 572 hadi 6000 katika kipindi cha mwaka huu ukilinganisha na kipindi kama hichi kwa mwaka jana.