Ajali ya kwanza ya kusababishwa na Gari linalojiendesha la Google imeripotiwa kutokea mwezi uliopita katika eneo la Mountain View huko jijini California. Japokuwa zimekwisha tokea ajali kadhaa zilizohusisha magari haya, hii ni mara ya kwanza kwa gari hilo la Google kuwa ndio chanzo cha ajali.
Ingawa bado ripoti ya trafiki haijatoka kuonesha nani anamakosa, tayari Google katika ripoti yake ya mwezi wameeleza chanzo cha ajari hiyo.
Ripoti inasema kwamba ajali hiyo ilitokea wakati gari hilo linalojiendesha lenyewe lilipokuwa linajaribu kukwepa kizuizi barabarani, baada kuingia katika njia ya basi kubwa software ya gari hilo ilitegemea kwamba basi lile lingeipisha lakini basi halikuipisha na kupelekea kukwanguana huko.
Hakuna ambaye ameumia katika ajali hii lakini hata hivyo kama ripoti ya trafiki itaonesha kwamba gari hili linalojiendesha ndio lenye makosa basi itakuwa ndiyo ajali ya kwanza kusababishwa na gari hili linalojiendesha baada ya kufanyiwa majaribio ya muda mrefu.
Wakati ajali hiyo inatokea dereva wa majaribio ambaye anatakiwa kuchukua usukani pindi anapooona kwamba gari hilo linataka kwenda mrama anasema aliliona basi hilo likija lakini alitegemea kwamba basi lingesimama ama kupunguza mwendo kupisha gari hilo la google kupita.
Msemaji wa Google alisema kwamba software inayoendesha gari hilo itabadilishwa kufuatia tukio hilo ili kuiboresha, hii inatokana na ukweli kwamba magari makubwa na mabasi ni ngumu kupisha magari madogo barabarani hivyo kupelekea ajali kama hii kutokea.
Google inatumia magari kutoka makampuni ya Toyota Audi na Lexus kwa kuyawekea mitambo ya kujiendesha na mpaka mwezi wa tisa mwaka 2015 Google walikuwa wamekwisha yajaribu magari yao umbali wa kilomita 1,948,394. Katika umbali huu ni magari 25 tu ya Google amabayo yalihusika na ajali 14 mbalimbali ambazo kwa mujibu wa Google hazikuwa zimesababishwa na magari yao yanayojiendesha.
Tunazidi kuona maboresho na ukuaji wa teknolojia ya magari yanayojiendesha yenyewe huku makampuni yaliyojikita katika utengenezaji wa teknolojia hiyo wakidai magari yanayojiendesha yapo salama zaidi ukilinganisha na kama mtu akiwa ndiyo dereva. Je una maoni gani? Tuambie