Kama wewe ni mtumiaji wa WhatsApp basi tayari utakuwa umeona ujumbe unaosambaa ukidai kama umepoteza simu yako basi tuna namba ya IMEI kwenda cop@vsl.net. Je kuna ukweli wowote?
Hapana. Si Kweli.
Katika ujumbe huo unaosema hakuna ulazima wewe kwenda kutoa ripoti polisi unadai ukituma taarifa zako kadhaa na namba ya IMEI ya simu yako kwenda kwenye barua pepe hiyo utapata msaada wa kutafutiwa simu yako.
Historia
Uongo huu una zaidi ya miaka minne sasa hivi na ushasambazwa katika mataifa mbalimbali. Ila miaka ya nyuma ilikuwa ni ya kweli ila kwa mkoa/jiji flani tuu huko India. Barua pepe hiyo ilikuwa cop@vsnl.net na ilikuwa inamilikiwa na kituo cha polisi cha Chennai huko India, na ni kweli ilikuwa inatumika kwa ajili ya kutoa huduma ya simu zilizopotea kwa wananchi wa jimbo hilo tuu.
Baada ya hatua kupata umaarufu ndio ikaanza kusambazwa hovyo hadi nje ya jimbo hilo na katika mataifa mengine – polisi wa jimbo wakaachana na anwani hiyo. Uongo ukazidi kukua na kubadilishwa hadi sasa ujumbe unaosambazwa ni ule ule ila barua pepe imebadilishwa na sasa ni cop@vsl.net badala ya ile ya cop@vsnl.net.
Teknokona tunapenda kukutaarifu ya kwamba huduma hiyo haipo na usiingie kwenye kundi la kuzidi kusambaza na kama umeona ujumbe umetumwa basi ni bora uwape taarifa sahihi ndugu na marafiki.
Nini kinaweza kutokea mtu akituma taarifa zake?
Kwa sasa ni ulimwengu wa data na udukuzi wa kufanikisha mambo mbalimbali ya kimtandao. Mtu kutuma taarifa zake muhimu kwenda kwenye barua pepe isiyo salama na isiyo rasmi ni sawa na upigiwe simu na mtu usiyemfahamu na ukubali kumpa taarifa zako binafsi – namba za simu, makazi, barua pepe, namba ya simu, IMEI, na nyinginezo.
Taarifa hizi zinaweza kutumika katika udukuzi wa kimtandao au kuunganishwa katika huduma za kimatangazo yasiyo ya lazima.
- Simu yako ikipotea na huku unakumbukumbu na IMEI namba zake toa taarifa polisi muda unaokwenda kutoa taarifa za kupatiwa laini mpya – ‘Renew’
- Jeshi la Polisi Tanzania lina uwezo mkubwa siku hizi wa kufuatilia na kukusaidia kuipata simu iliyoibiwa kama utatoa taarifa kwa wakati. Inaweza kuchukua muda kiasi, kwa sababu lazima simu itumike, ila uhakika wa kuipata kama mwizi au mtu ataitumia ni mkubwa sana.