Je unaweza kuamini ya kwamba nusu ya ajira zote kuchukuliwa na kompyuta ndani ya miaka 15 ijayo? Haya ni maneno ya muwekezaji mmoja wa masuala ya teknolojia kutoka China.
Bwana Kai-Fu Lee ambaye ni mwandishi, muwekezaji na pia ni mkurugenzi kwenye kampuni ya Teknolojia ana historia ya kazi ya zaidi miaka 30 katika masuala ya akili kompyuta – yaani AI (Artificial Intelligence).
Bwana Lee ashafanya kazi kama rais msaidizi kwenye shirika la Google, pia ashakuwa rais wa Google nchini China. Nje ya hapo ashafanya kazi pia Microsoft na Apple. Kampuni yake imekeza mabilioni ya dola katika makampuni madogo kwa makubwa ya ubunifu wa kiteknolojia.
Akiojiwa na televesheni ya CBS ya nchini Marekani, Bwana Lee amesema ana wasiwasi mkubwa ya kwamba mifumo ya elimu ya sasa isipobadilika na kuandaa kizazi kijacho kwa suala hili basi huko mbele vijana watapata tabu katika soko la ajira.
Amedai asilimia 40 ya ajira zitaweza kufanywa kwa ufanisi zaidi na mifumo ya kikompyuta. Ajira zinazoongoza kwenye orodha ni zile ambazo roboti anaweza kuzifanya, hizi ni kama vile utafutaji masoko kwa njia ya mawasiliano, huduma kwa wateja, wafanyakazi ndani ya magodauni – kazi za upangaji na utoaji mizigo, upokeaji na utunzaji wa pesa (cashiers), wahudumu katika migahawa na wasafishaji vyombo.