Serikali ya jimbo la California nchini Marekani imesema inategemea uwepo wa magari yanayojiendesha yenyewe bila dereva ndani kufikia mwezi Aprili mwaka huu.
Kwa muda mrefu makampuni yanayofanya majaribio ya magari yanayojiendesha yenyewe yamekuwa yakikutana na hitaji la kisheria la Calfornia ya kwamba lazima ndani ya magari hayo kuwe na dereva mwanadamu – kama ‘backup’, kama ikitokea mfumo wa kujiendesha wenyewe ukiwa na hitilafu.

Ila sasa serikali hiyo imekubali kukubali utumiaji wa teknolojia ya ‘remote human operator’, yaani kuwa na mtu aliyekwenye kituo flani akiwa na uwezo wa kufuatilia gari linalojiendesha lenyewe kupitia huduma ya intaneti na hivyo kuweza kulipokonya gari hilo uendeshaji na mtu huyu kuweza kuliendesha gari hilo ingawa yupo sehemu nyingine kabisa.
Hitaji hili ni muhimu kwa makampuni yanayotengeneza magari yanayojiendesha yenyewe kama Google kupitia kampuni yake ya Waymo, na pia kampuni ya General Motors, ambao wote wanalenga kuweza kuyauza magari hayo ata kwa makampuni yanayotoa huduma za taksi kama vile Uber.

Uwepo wa magari haya inamaanisha makampuni ya huduma za taxi yataweza kupunguza gharama kwa kuondoa uhitaji wa madereva katika magari na hivyo mtu mmoja atakayekuwa ofisini atakuwa na uwezo wa kufuatilia ata magari 5 – 6 yanayojiendesha yenyewe na kuingilia kati kama mfumo (AI – Akili feki ya gari) itakuwa na shida.
Teknolojia ya ‘remote control’ kwa vifaa kama magari tayari inatumiwa na mashirika mengine Marekani kama vile NASA na jeshi la nchini Marekani.
Google na General Motors si makampuni pekee yanayotarajiwa kunufaika na mabadiliko haya ya sheria kwa jimbo la California, wengine watakaonufaika ni pamoja na Nissan, Waymo, Phantom Auto na mengine mengi yanayojihusisha na teknolojia za magari yanayojiendesha.
Chanzo: TheDrive na tovuti mbalimbali