Teknolojia mpya ya FaceID katika toleo jipya la Simu janja ya kampuni ya Apple la iPhone X limemvuruga mwanamichezo nguli wa mieleka (wrestling) wa Marekani Jonh Cena.
Katika simu ya iPhone X, Kampuni ya Apple imefanya mabadiliko ya kuweka ‘lock’ mpya ya Face ID badala ile ya Touch ID.
Teknolojia hii itamuwezesha mtumiaji kufungua simu yake kwa kutambuliwa kwa uso wake badala ya kuweka kidole kama ilivyokuwa kwa simu za iPhone za matoleo mengine.
Teknolojia hii ndiyo iliyomkwanza mwanamieleka huyo wa marekani ambaye amekuwa akitumia maneno ya “You can’t see me” (Huwezi kuniona) hasa pale anapompiga mpinzani wake katika ulingo wa mieleka.
Msemo huo umekuwa maarufu kwa watu wengi duniani hususani wale wanaomfatilia John Cena na mchezo huo wa mieleka. John Cena anatajwa kuwa mmoja wa wanamieleka maarufu na wenye wapenzi wengi katika mchezo huo.
Muda mfupi baada ya uzinduzi wa iPhone X, John Cena alitwiti katika akaunti yake ya Twitter kwa kuandika “Soo #iPhoneX about #FaceID…ummmmm…what do I do? akimaanisha (tafsiri isiyo rasmi) kwamba “kwa hiyo, iPhoneX kuhusu FaceID nifanyeje?”
Kama John Cena ataamua kumiliki simu ya iPhone X atalazimika kuweka uso wake kama ‘Lock’ ya kufunga na kufungulia simu. Hivyo ule msemo wake wa ‘You cant see me’ utakuwa hauna maana yoyote mbele ya Face ID ya iPhone X.