Programu endeshi ambayo inashauriwa kutumika kwenye kompyuta katika miaka ya karibuni ni Windows 10 lakini lazima tufahamu kuwa si kila kipakatalishi kinakubaliana toleo hilo (Windows 10) hivyo ni vyema ukazingatia mambo kadhaa muhimu ili kifaa chako kiweze kufanya kazi vyema.
Kwa miaka mingi tuu sasa nimekuwa mpenzi wa Windows 10 na mara kwa mara nimekuwa nikikutana na changamoto mbalimbali ambazo zilihitaji kuumiza kichwa ili kuweza kuzitatua. Juzi juzi tuu nililetewa kompyuta ambayo ilikuwa imewekwa katika mfumo wa tabiti hivyo kufanya kuwa shida kwa mhusika kuweza kuitumia kama alivyozoea. Sasa swali la kwanza kujiuliza “Mfumo wa tabiti kwenye Windows 10 ukoje?”. Je, inawezekanaje kuuwasha au kuuzima?
Mfumo wa tabiti kwenye Windows 10
Kama unafahamu jinsi ambavyo programu zinakuwa zimejipanga kwenye iPad au tabiti nyinginezo basi ni hivyo hivyo zinavyokuwa tukizungumzia Windows 10 na kiukweli inaleta ugumu kidogo mtu kuweza kutumia kompyuta iliyo katika mfumo husika ilihali yeye amezoea ule ambao ni rafiki/uliozoeleka. Kutafuta programu unayotaka basi inabidi ubofye kipengele namba 3 (all apps) upande wa kushoto juu.
Jinsi ya kuweka/kuondoa mfumo wa tabiti kwenye Windows 10
Inawezekana kabisa wakati unatumia kompyuta (yenye Windows 10) ukabonyeza sehemu halafu mpangilio wa programu ukabadilika kabisa hivyo kusababisha ugumu wa kutumia kifaa husika. Ukiangalia pembezoni upande wa kulia chini kwenye Windows 10 utaona kiboksi kidogo. Sasa ukibofya kwenye kiboksi husika utakutana taarifa fupi (kama zipo) lakini pia kwa upande wa Kusini kipengele cha kwanza kabisa kutoka kushoto ni “Tablet mode” na ukikiwasha/kukiruhusu basi mpangilio mzima wa programu utabadilika na kuwa sawa kama kwenye tabiti.
Ni matumaini yangu makala hii itakuwa msaada kwa yeyote ambaye anatumia Windows 10 kisha akakumbana na changamoto niliyoielezea. Usisite kuwashirikisha wengine na daima kumbuka kutembelea tovuti yetu kwa habaro mbalimbali zinazohusu teknolojia.
Chanzo: Microsoft
No Comment! Be the first one.