Teknolojia inarahisisha mengi sana….Hivi karibuni watumiaji wa simu Tanzania wataweza kuwa na uwezo wa kupima ubora wa udongo wa eneo lolote kwa kutumia simu zao.
Teknolojia hii inaletwa na kampuni kutoka Kenya inayofahamika kwa jina la Capture Solutions.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo aliliambia gazeti la The Citizen ya kwamba wanategemea kufikia mwezi wa tisa mwaka huu wataweza anza rasmi kuuza teknolojia yao Tanzania.
Hili linawezekanaje?
Hili linafanikishwa kupitia app yao utakayoweka kwenye simu yako na pia kupitia kifaa kingine ambacho ndicho utaweka udongo ndani yake na kisha kuunganisha kifaa hicho na simu yako.
Kifaa hicho pia kinakuja na eneo la kuweka memori kadi kwa ajili ya kuhifadhia data na pia kuweza kuhamisha data zinazopatikana.
Tanzania wanafahamika kama Capture Solutions Tanzania LTD
Kampuni hiyo imeshafungua tawi hapa Tanzania na inajivunia mafanikio kwa kuwa na wateja takribani 200,000 nchini Kenya wanaotumia simu zao kwa ajili ya huduma za aina hii kutoka Capture Solutions.
Je soko lipo? Kwa kiasi kikubwa naamini soko lipo, kilimo ni moja ya shughuli kubwa kabisa ya kiuchumi nchini na kama watajipanga vyema basi haitashangaza kama watafanikiwa hapa nchini pia.
Gharama pia ni jambo la kuangaliwa, TeknoKona itaendelea kufuatilia ujio huu na kukupasha pale taarifa zaidi zikipatikana.
Chanzo: TheCitizen