Xiaomi ni kampuni ya vifaa vya elektroniki inayokua kwa kasi zaidi duniani. Na sasa Xiaomi wawatania Apple kwa kuuza vipakatalishi, simu, pamoja na saa janja kwa mafungu yaliyobeba majina ya simu mpya za iPhone.
Ni hivi karibuni tuu shirika la data za kimauzo – IDC lilionesha ya kwamba Xiaomi imeshika nafasi ya nne kwenye soko la simu kufikia Agosti 2018. Takwimu hizo zimeonesha kampuni ya Xiaomi imepanda kwa kasi katika soko la simu. Kufikia kipindi cha nusu cha mwaka huu kampuni hiyo imefikisha umiliki wa soko la simu kwa asilimia 9, na hivyo kuifanya kuwa nyuma ya makampuni matatu tuu: Samsung, Huawei, na Apple.
Siku chache zilizopita Apple wametambulisha simu zao mpya zilizobeba majina ya iPhone XR, iPhone XS na iPhone XS Max. Bei za simu hizo ni $749|Tsh. 1,722,700 kwa iPhone XR, $999|Tsh. 2,297,700 kwa iPhone XS na $1,099|Tsh. 2,527,700 kwa iPhone XS Max.
Xiaomi wametumia majina hayo hayo pamoja na bei hiyo hiyo kuna na mafungu ya bidhaa ambazo unaweza zipata kutoka Xiaomi kwa bei hiyo hiyo ya iPhone moja kutoka Apple.
> iPhone XR = Xiaomi XR (Kwa takribani Tsh 1,700,000/=)
Kwa Xiaomi kwa bei sawa na iPhone XR moja, utapata Mi Notebook Air, Mi Band 3 pamoja, Headphone ya Mi Bluetooth Mini pamoja na simu ya Xiaomi Mi 8 SE.
Sifa za Xiaomi Mi 8 SE: Inakuja na Android Oreo, betri la mAh 3120, RAM ya GB 4 pamoja na diski ujazo wa GB 64. Kamera ni ya megapixel ya 12, na huku ya selfi ikiwa megapixel 20.
> iPhone XS = Xiaomi XS (Kwa takribani Tsh. 2,300,000/=)
Kwa bei ile ile ya iPhone XS utapata simu janja ya Mi Mix 2S, laptop ya Mi Notebook Air, Mi Band 3, pamoja na headphone ya Mi Bluetooth Mini.
Sifa za Xiaomi Mi Mix 2S: Ilitambulishwa rasmi mwezi Machi 2018, ina kioo cha inchi 5.99, inakuja na RAM ya GB 6 huku ikiwa na diski uhifadhi wa GB 64. Pia inakamera ya Megapixels 12 na huku kamera ya selfi ikiwa ni ya megapixel 5. Betri ni la mAh 3400.
> iPhone XS Max = Xiaomi XS Max (Kwa takribani Tsh. 2,500,000/=)
Hapa unapata laptop ya Mi Notebook Pro, simu ya Xiaomi Mi 8, Mi Band 3 pamoja na headphone ya Mi Bluetooth Mini.
Kwa uchache, sifa za Xiaomi Mi 8: Ilitambulishwa mwezi Mei 2018. Inaukubwa wa inchi 6.21, ikiwa na RAM ya GB 6 na huku diski uhifadhi ikiwa ni ya GB 64. Betri ni la mAh 3400, huku kamera ikiwa ni ya megapixel 12, huku ya selfi ikiwa ni ya megapixel 20.
Watafiti wengi wanaamini haitachukua muda mrefu kwa Xiaomi kufikia namba 2 au 1 katika soko la simu duniani. Tayari katika mataifa kama India Xiaomi wanashindana moja kwa moja na Samsung.