Serikali ya nchi ya venezuela Alhamisi imesema kuwa shambulizi kubwa la kimtandao (Cyberattack) lililotokea mapema wiki hii limeathiri watumiaji simu za mkononi milioni saba kwa kukosa huduma.
Kikundi kinachojiita The Binary Guardians kimedai kuhusika na shambulio hilo la kimtandao kwa kusema shambulizi hilo lililenga Tovuti za serikali, mahakama, Tume ya uchaguzi na Bunge la nchi hiyo.
“Nia yetu ni kutoa tumaini kwa watu bila kujali nguvu ya adui inayoonekana, kwamba kuna nguvu katika umoja,” ilinukuliwa barua pepe kutoka katika kikundi hicho juu ya shambulizi la kimtandao Venezuela.
Shambulizi hilo ambalo liliharibu takribani Tovuti 40 za serikali, limedaiwa kufanywa na Kikundi hicho kuonesha hasira kwa kile kinachodaiwa kupinga ‘udikteta’ wa Rais Nicolas Maduro wa nchi hiyo.
Katika tovuti za serikali zilizodukuliwa zilionesha maneno yaliyosema ‘Operesheni David’ na Kipande cha picha kutoka filamu ya The Great Dictactor ya Charlie Chaplin.
“Hivi ni vitendo vya kigaidi vilivyoathiri kampuni ya Movilnet jumatano na kuacha mikoa saba bila ya mawasiliano na watu milioni saba kukosa huduma”, alisema Waziri wa Sayansi na Teknolojia Hugbel Roa.
Venezuela ina makampuni mawili binafsi yanayotoa huduma za mawasiliano nchini humo ambayo ni Digitel na kampuni ya inayomilikiwa na Spain ya Movistar.
Wazir Roa alisema mashambulizi hayo yalianza Jumatatu ambapo Tovuti kadhaa za serikali na makampuni binafsi zilidukuliwa.