Tayari habari ya ujio wa kivinjari cha Microsoft Edge kinachotengenezwa kwa kodi ya msingi ya Chromium ilitangazwa na Microsoft. Toleo la beta la kivinjari hichi limevuja na sasa linapatikana mtandaoni.
Chromium ni mradi wa utengenezaji wa kivinjari huru kinachokuja na teknolojia za kisasa zaidi za mtandao. Mradi huu unasimamiwa na Google na unahusisha wadau wengine wowote wanaojisikia kuchangia. Kupitia toleo la Chromium ndio Google anaboresha na kuingizia manjonjo kadhaa kuleta toleo la Google Chrome. Kwa wengi uamuzi wa Microsoft unaonesha Google imeshinda kiteknolojia katika eneo la teknolojia za vivinjari.
Microsoft hatakuwa wa kwanza kuachana na utengenezaji binafsi wa kivinjari na kutegemea kivinjari kikuu cha Chromium katika kuleta toleo lake la Kivinjari cha Edge, tayari miaka mingi sasa ata kivinjari cha Opera kinatengenezwa juu ya misingi ya Chromium.
Sifa na uwezo wa toleo la Edge havijaenda mbali na sifa zilizokuwa zinategemewa kuwepo kwa kivinjari kinachotengenezwa juu ya kivinjari mama cha Chromium. Kivinjari cha Edge sasa kitaweza kukubali ongezeka la uwezo (extensions) kwa kupakua plugins kutoka moja kwa moja kwenye soko la Chrome la Google – ingawa pia kutakuwa na soko la extensions la Microsoft.
Kikubwa wamechukua Chromium na kuipa muonekano mzima wa programu za Windows na kuweka huduma zake za Microsoft kuwa ndio huduma kuu – hii ni pamoja na huduma za kuhifadhi kumbukumbu n.k.