Simu hizi zimepotea na kurudi mara kadhaa kwenye soko, baada ya mafanikio kadhaa ya hivi karibuni TCL na kampuni ya BlackBerry inaonekana wameshindwa kuendeleza mahusiano tena.
Kupitia akaunti ya Twitter ya BlackBerry Mobile, tangazo liliwekwa likisema TCL wataacha rasmi uuzaji wa simu za BlackBerry kufikia mwisho wa mwezi Agosti mwaka huu. Ila wataendelea kutuma masasisho na huduma nyingine zozote muhimu hadi Agosti mwaka 2022.

Kilichotokea:
- TCL walitangaza rasmi Disemba 2016 kupewa hakimiliki ya biashara za simu na haki ya kutumia jina na teknolojia za BlackBerry kwenye simu hizo.
- Jambo hili lilifanywa na kampuni mama ya BlackBerry baada ya wao wenyewe kujaribu mara kadhaa kuleta simu bila mafanikio – hazikufanya vizuri sokoni. Baadae wakaona bora kuingiza mapato kupitia kuuza hakimiliki hiyo huku wao wakiendelea kujikita katika biashara kubwa zaidi za kiusalama wa teknolojia za kimawasiliano hasa hasa kwa makampuni.
Mpaka sasa TCL walishakuja na simu mbalimbali zilizobeba jina la BlackBerry, hii ni pamoja na BlackBerry KeyOne mwaka 2017, na BlackBerry Key 2 mwaka 2018.
Tayari TCL walianza kuirudisha simu ya BlackBerry kwenye sifa nzuri hasa hasa kwa sasa ikiwa inakuja na programu endeshaji ya Android.
Kuna watafiti wanaosema uamuzi wa BlackBerry unaweza kuchangiwa na wao kuona uamuzi wa TCL pia kuendelea na uwekezaji wa utengenezaji wa simu zao zinazoenda kwa jina la Alcatel. Uamuzi huu unaweza ukawa umewafanya BlackBerry kuona TCL hawataendelea kuzipa simu zinazokuja na jina la BlackBerry nafasi nzuri katika uwekezaji na utengenezaji.