Shirika la ndege la Uingereza limekumbwa na msukosuko baada ya kupatwa na tatizo la kompyuta katika viwanja viwili vya ndege vikubwa jijini London.
Shirika la ndege la Uingereza limethibitisha kwamba tatizo hilo sio kwa sababu ya udukuzi ama makosa ya kimtandao bali linatokana na kushindwa kufanya kazi kwa kifaa.
Tatizo hili limedhuru mtandao wa kampuni hiyo, app yake ya simu na pia vituo vyote vya simu vya kampuni hiyo. Kimsingi hakuna ndege iliyoweza kutua ama kuruka katika viwanja hivyo viwili kwa kuwa mtandao wa kukagua mizigo na kuwakagua abiria haufanyi kazi kufuatia tatizo hili.
Tukio hili limepelekea Shirika hilo la ndege kusitisha zaidi ya safari 1000 za ndege kwenda sehemu mbalimbali duniani siku ya jumamosi. Hatahivyo wataalamu wa usafiri wa anga wanadai kwamba itachukua siku tatu mpaka nne kwa shirika la ndege Uingereza kufanikiwa kurudisha hali ya kawaida.
Lawama mwisho wa siku zinarudi kwa shirika la ndege Uingereza kwa kutokuwa na mpango mbadala madhubuti ambao ungeweza kusaidia katika kipindi hiki ambacho mfumo wa mtandao haufanyi kazi. inategemewa kwamba tukio hili litafanya mashirika ya ndege kufikiria njia mbadala za kuendesha shughuli zake pindi njia za kawaida zitakaposhindwa.
Wakati makala hii inachapishwa tayari tatizo hili limetatuliwa na shughuri zimerudi katika viwanja hivyo viwili huko London.