Je umeshawahi kusikia kuhusu C919? Kama ni msomaji wa Teknokona wa muda mrefu basi utakuwa unakumbuka tulishaandika kuhusu harakati za China za kuja na za ndege za abiria za kushindana na ndege za makampuni ya Boeing (Marekani) na Airbus (Ulaya).
Baada ya kufanya majaribio kadhaa ya ndege hizo bado mradi huo upo nyuma kwa muda kufikia hatua za kupata leseni ya kuruhusu ndege hizo kuanza kuuzika kwa wateja. Taarifa zinasema bado wahandisi wa shirika la kiserikali la Commercial Aircraft Corporation (COMAC).
Hadi sasa ndege hiyo imekamilisha moja ya tano tuu ya idadi nzima ya majaribio yanayoitajika ili ndege kupata kibali cha kuuzwa na kutumika na abiria. Kwa China ndege inatakiwa ifikie majaribio yanayohusisha idadi ya masaa 4,200 angani ili kuweza kupata kibali cha kuuzwa na kutumika na abiria.
Serikali ya China inawekeza kwa kasi katika eneo hili wakiwa na lengo la kuweza kuleta ushindani na kutotegemea ndege kutoka Boeing na Airbus. Nchi ya China ni soko kubwa la ndege za abiria kwa sasa kutokana na maendeleo makubwa ya kiuchumi, ukubwa wa nchi na wingi wa majiji ya kisasa yanayochangia biashara na ukuaji wa sekta ya usafiri wa anga.
Data zinaonesha kufikia mwaka 2028, soko la usafiri wa ndani wa anga nchini China utakuwa mkubwa kuliko taifa lolote duniani. Makampuni ya ndani ya China pia yamezidi kukua katika soko la safari za kimataifa kati ya China na mataifa mengine. Kwa mwaka 2014 ni makampuni 12 tuu ya China yalikuwa na safari za kimataifa kuunganisha China na mataifa mengine, kufikia mwaka 2019 idadi iliongezeka kufikia makampuni 29.
Serikali ya China inawekeza kwenye uweze wa utengenezaji wa ndege nchini China si tuu kwa ajili ya soko la China bali pia kwa ajili ya soko la dunia. Kupitia mkakati wao wa ‘Made in China’ serikali imeweza kuwekeza katika teknolojia mbalimbali ili kuliwezesha taifa hilo kutokuwa tegemezi kwa teknolojia na bidhaa kutoka nje.
Je watafanikiwa?
Watafiti wanaona ndani ya miaka minne hadi mitano COMAC watafanikiwa katika kuboresha ndege hii, na suala la kuchelewa ni jambo linalotokea kwenye programu nyingi za kuleta ndege mpya – ata kwa Boeing na Airbus. Tofauti tuu ni kwamba COMAC inawachukua muda zaidi kwa kuwa bado ni kampuni changa.
Cha kuboreshwa
Maeneo mengi ya ndege hiyo yashakamilika. Kikubwa ni kuboresha uwiano wa nguvu ya injini, na ubora wa bodi nzima ya ndege. Ndege hizi zinakuja na injini za kisasa kutoka kampuni ya CFM International, hawa ni watengenezaji maarufu wa injini za ndege zinazotumika ata kwenye baadhi ya ndege za Boeing na Airbus).