Kulingana na ripoti ya Strategy Analytics kampuni ya Apple imeendelea kuongoza mauzo ya simu zake janja kwa soko la nchi ya Marekani katika robo tatu ya mwaka 2017.
Hata hivyo mauzo ya simu hizo yameshuka kulingana na ya mwaka jana ambapo mwaka huu waliuza simu milioni 12 na mwaka jana milioni 13 kwa robo ya tatu ya mwaka. iPhone 8 na iPhone 8 Plus zimeonekana kupata changamoto za mauzo kwa kuwa watu wengi walikuwa wanasubiri iPhone X ambazo zimeanza kuuzwa Novemba 3 katika soko la Marekani.
Samsung iliendelea kuwa nafasi ya pili kwa kusafirisha simu milioni 9.9 sawa na asilimia 25 ya soko lote la marekani na mauzo hayo yamepanda kulingana na mwaka jana walipouza simu milioni 9.7 katika robo tatu ya mwaka.
Licha ya kuwa nafasi ya pili kwa soko la Marekani lakini Samsung ndio inaongoza kwa mauzo duniani kote. Simu za LG, ZTE na Motorola zilikuwa kati ya nafasi tano za juu katika soko la mauzo. Mauzo ya Motorola yaliongezeka mara mbili kutoka milioni 1.1 mpaka milioni 2.1 na hivyo kuwa na asilimia 5 ya mauzo kwa soko la Marekani.