Zaidi ya muongo mmoja uliopita simu za Motorola zilikuwa kwenye masikio ya watu lakini umaarufu wake ukashuka maradufu ila mwaka 2018 unaweza ukawa mwaka wa kuitengenezea ramani nzuri kwenye soko la ushindani.
Lenovo ambao ndio wanamiliki jina na bidhaa za Motorola wapo mbioni kutambulisha simu rununu waliyoiita Motorola One Power. Ni simu ambayo ilikuwa na minong’ono mingi na hatimae sifa zake zimevuja.
Sifa za Motorola One Power zilizojulikana kabla ya kuzinduliwa kwake.
Kwa haraka haraka ni simu janja ambayo imedhamiria kuleta ushindani katika soko la simu rununu kwani ina vitu kadha wa kadha vinavyovutia. Motorola One Power inaaminika kuwa na sifa zifuatazo:-
Kioo: Kioo chake kinaaminika kitakuwa na ukubwa wa inchi 6.2 (1080×2280 pixels) kinachoonyesha picha ang’avu kabisa au kwa lugha iliyozoeleka FULL HD.
Prosesa na kamera: Motorola One Power itakuwa na Qualcomm Snapdragon 636 SoC. Inatarajiwa kuwa na kamera mbili nyuma; moja ikiwa na MP 12 na nyingine ikiwa na MP 5. Kamera ya mbele pia itakuwa na MP 8.
RAM na Diski uhifadhi: RAM yake itakuwa ya GB 4 huku diski uhifadhi ukiwa GB 64.
Programu endeshi na betri. Motorola One Power inaelezwa sana kuwa itakuwa na uwezo wa kupokea toleo la Android One hivyo inaaminika kuwa itakuja na Android 8.1. Betri yake inategemewa kuwa na 3,870 mAh.
Bei yake bado haijajulikana mpaka hapo itakapotambulishwa kwa ulimwengu lakini inaaminika kuwa ni simu janja ambayo itakuja kushindana vilivyo na Xiaomi Redmi Note 5 Pro.
Vyanzo: First Post, Gadgets 360
One Comment
Comments are closed.