Je ushawahi kukutana na simu ya iPhone refurbished? Kama jina linakuchanganya simu za iPhone zenye sifa hii ni zile simu unazokuta zinauzwa kwa bei nafuu zaidi na huku zikiwa na muonekano wa kuwa mpya kabisa.
Asilimia kubwa ya simu za iPhone zinazouzwa nchini hasa hasa kwenye maduka maarufu maeneo ya Sinza, Kijitonyama na ata sehemu zingine ni simu ambazo zinasifa ya kuwa ‘refurbished’.
Kwa bei zinaweza zikawa zinauzwa kwa bei ya chini kwa takribani laki nne hadi sita ukilinganisha na simu hiyo hiyo ukinunua katika maduka rasmi – Apple iStore.
-
iPhone mpya – Hizi zinauzwa na Apple, zinakuja na boksi lenye kila kitu. Pia utapata waranti ya muda flani.
-
iPhone refurbished – Hizi zinauzwa na Apple, au wafanyabiashara wengine mbalimbali
-
iPhone used – Hizi zinauzwa na watu binafsi
Je kwa nini simu hizi huwa zinauzwa kwa bei nafuu sana?
Simu hizi zinakuwa ni simu ambazo zilishauzwa kwa mteja na zikapata tatizo na hivyo kurudishwa kiwandani. Zinaporudishwa zinafanyiwa mabadiliko kwa kuingiza vipuli vipya au vipuli vizima kutoka kwenye singine za iPhone zilizorudishwa baada ya kutumika kwa muda mfupi.
Kivipi zinarudishwa?
- Simu inaweza ikawa imenunuliwa na kisha ikapata tatizo la kiufundi, basi mtumiaji kwa kuwa anakuwa bado kwenye waranti anaweza kuirudisha Apple na kupewa simu nyingine mpya. Simu aliyorudisha itarudishwa kiwandani, kurekebishwa na kisha kuuzwa kama refurbished iPhone.
- Uharibifu wa kuvunjika n.k, kuna wanaonunua simu mpya na kisha zikapata ajali flani. Kwa kuwa wanakuwa katika bima wanaweza kuzirudisha na kisha Apple huzirudisha kiwandani zinarekebishwa na kisha kurudishwa sokoni kwa mfumo wa refurbished.
Je ni salama?
Simu hizi Apple wanasema zinapitia majaribio yote ya ubora kama simu mpya baada ya kufanyiwa matengenezo. Hii ina maana kwa kiasi kukubwa kiubora tofauti kuu inakuwa zenyewe zishawahi kutumika. Apple huzifanyia mfumo wa ‘burn-in’ ambao unahusisha simu hizi kuwekwa upya programu endeshaji na kupatia namba mpya za utambulisho – serial number & part number.
Kati ya simu refurbished na simu mpya kabisa – hakuna tofauti ya ufanisi kiutendaji.
Sehemu nyingine ni kwamba pia kuna kampuni zingine pia China zinafanya biashara hii ya kufanyia matengenezo iPhone zilizotumika. Tofauti kuu kati ya refurbished za Apple na hizi za watengezaji wengine ni suala la kupata serial number mpya na pia kupewa sifa ya ‘Apple Certified Refurbished Product’. Yaani kwa zile za Apple bado zinapata sifa ya waranti na dhamana, sifa ambayo huwa wanazipa ata simu zao mpya.
Pia kuna wafanyabiashara wengine hununua simu za refurbrished kwa jumla moja kwa moja kutoka Apple na kisha kuziuza bila baadhi ya sifa kama waranti na dhamana.
Ukiwa na wasiwasi kuhusu simu unayotaka kununua au umekwishanunua, unaweza kuangalia kama simu au laptop ya Apple unayotumia imekidhi ubora au ina waranti au dhamana kwa kutumia hii linki – https://checkcoverage.apple.com/ ( Chukua serial number ya simu yako kupitia Settings -> General -> About -> Serial Number)