IP Address . Najua inaweza ikawa sio mara yako ya kwanza kulisikia hili neno katika ulimwengu wa teknolojia. Pengine huwa tunalisikia na hatuelewi maana yake? sio dhambi kutoelewa lakini leo naomba TeknoKona ikujuze juu ya hili..
Unajua bwana, haya mambo bwana! yaani siku hizi ukitaka kuingia mtandaoni sio lazima uwe unajua makorokoro mengi, ni kuchukua kifaa chako tuu kama ni simu au kompyuta alafu unazama tuu. Nadhani hii ni tofauti na zamani ambapo ilibidi lazima uwe na ujuzi fulani hivi.. nazungumzia kabla hata ya simu janja
Ili kuingia katika mtandao wowote ni wazi kuwa kuna baadhi ya mambo yafanyike ili kukuunganisha na mtandao husika unaoutaka katika haya mambo moja wapo ni IP Address.
IP Address Ni Nini?
Ni swali zuri sana kujiuliza na leo TeknoKona itahakikisha umeelewa maana halisi ya jambo hili
Kila mara kifaa kinpoingia katika mtandao ni lazima kitafute IP Address ya mtandao husika na huku nyuma bila ya kusahau kifaa hicho pia kinakua na IP Address yake chenyewe. Kwa kifupi hii ni sawa sawa na utambulisho wa kifaa husika. Hivyo basi ili kuwasiliana katika mtandao ni lazima vifaa hivi vijuane kwa utambulisho (IP Address) hii itasaidia kifaa kupata taarifa sahihi ambayo inaomba.
Chukulia mfano upo na kompyuta yako na umeandika www.google.com, kitakachofanya google watume kurasa zao kwako na wasitume katika kifaa kingine ni kupitia IP Address yako — Ambayo ndio namba ya utambulisho wa kifaa hicho.
Kuna aina mbili
- Aina ya kwanza kabisa na ambayo imezoeleka sana ambayo inajulikana kama IPv4 address
Aina hii ni ile ambayo inakua na namba nne ambazo zimetenganisha na doti (.). Namba yake ya kwanza ni lazima iwe kati ya kundi hili 1 na 191 na zile zingine zilizosalia lazima zima katikati ya 0 na 255. kwa mfano 81.151.203.58
- Aina nyingine iliyobakia inajulikana kama IPv6 na inaweza ikaonekana kama 2001:db8:0:1234:0:567:8:1
IP Address ina umuhimu mkubwa sana kwa sababu inaongea mengi sana katika intaneti na pia ndio inayokuwezesha wewe kuwasiliana. Fikiria IP Address ni kama nyumba, ili nije kwako kukulete tarifa fulani ni lazima niwe napajua kwako. Hivyo basi ili taarifa unayotaka kuipata kutoka katika mtandao ni lazima mtandao usome IP Address yako kwanza.
Jinsi Ya Kujua IP Address Ya Kifaa Chako
Kuna njia nyingi sana za kukuwezesha kujua kifaa unachotumia kina IP Address gani
Njia ya kwanza ni ile ambayo tumeizoea kila siku, ingia katika Google na kisha andika ‘Whats My IP Address’ na kisha Google itakupa jibu. Hii ndio njia nyepesi zaidi lakini vile vile unaweza ukatummia njia zingine kama vile kuingia katika mtandao wa whatismyip.com .
Kumbuka IP Address yako inaweza ikabadilika muda wote kutokana na kifaa unachutumia kuingia katika mtandao, kwa mfano IP Address ya simu na ya kompyuta yako lazima zitofautine.