Sahau teknolojia ya ‘notch’, kampuni ya Visionox ya nchini China yatengeneza kamera isiyoonekana kwenye display ya simu. Hii ni kwa kamera ya selfi.
Limekuwa lengo la muda mrefu kwa makampuni mengi kutafuta namna ya kufanya kamera ya mbele ya simu, ya selfi, kutochukua eneo kubwa la mbele/display ya simu. Samsung ambaye anatengeneza display za simu nyingi hii ikiwa ni pamoja na za iPhone wamekuwa wakifanya utafiti mkubwa ili kuwezesha jambo hilo.
Ujio wa ‘notch’, kuruhusu display kusambaa katika eneo kubwa la simu mbele huku kamera ikichukua kinafasi kitogo ilikuwa ni moja ya maendeleo ya kupunguza eneo la kamera.
Kupitia teknolojia ambayo Visionox wamefanikiwa kuitengeneza kamera ya simu itaweza kuwa chini ya display na hivyo kutoonekana kabisa juu ya simu yako na hivyo kuruhusu display kuchukua eneo lote la uso wa simu.
Kampuni ya Visionox sio ngeni na ni moja katika makampuni makubwa nchini China katika utengenezaji skrini za OLED. Wao ndio wamehusika katika teknolojia za display zinazotumiwa na Xiaomi.
Wameweza kufanikisha suala hili kupitia maboresho ya teknolojia ya OLED. Wamedai wamefanikiwa kuepusha kabisa upotevu wa ubora wa picha ambao ungeweza kuathiriwa kutokana na kamera kuwa chini ya display.
Wamesema tayari wamefanikiwa kufikia kiwango cha utengenezaji mkubwa na hivyo tutegemee muda si mrefu kuona simu zinazokuja na uwezo huo zikiingia sokoni. Katika wateja wake wakubwa ambaye anaweza kuonekana kuwa na uharaka wa kuitumia tusishangae ikiwa ni Xiaomi.
Vyanzo: Forbes na vyanzo mbalimbali