Kampuni ya simu ya Huawei ipo katika mpango wa kuhakikisha simu zake mpya kuja na apps 70 maarufu ili kuepuka vikwazo vya serikali ya Marekani vinavyowazuia kutumia huduma za Google ikiwa ni pamoja na soko la apps la Google PlayStore.
Tokea vikwazo vya Marekani dhidi ya kampuni ya Huawei viwekwe kwa sababu za ‘kiusalama’, tafiti zinaonesha mauzo ya simu za Huawei katika masoko ya nje ya China yameshuka ukilinganisha na kipindi cha nyuma. Ila wakati huo huo tofauti hiyo haijaonekana kwani wananchi wengi wa China wamejitokeza kununua zaidi simu za kampuni hiyo kama namna ya kuionesha wanaiunga mkono, na hivyo kwa ujumla wake bado hali ya mauzo haijawa mbaya.
Kampuni hiyo tayari ipo kwenye mchakato wa kuanzisha mfumo huru wa soko la apps huduma ambayo itawezesha makampuni mengine ya China kama vile OPPO, Xiaomi na Vivo kuweza kuunganisha app zao za masoko ya apps kwa urahisi na kuweza kupata apps kwenye masoko yao kwa urahisi. Huduma hiyo dhidi ya Google Mobile System inaenda kwa jina la Global Developer Service Alliance.
Wakati bado mfumo huo unafanyiwa kazi taarifa za uhakika zinaonesha kampuni hiyo imeaamua kuweka apps mbalimbali maarufu moja kwa moja kwenye simu zake kama njia ya kuepuka vikwazo vya kutumia Google Playstore na pia kuwawezesha wateja wao kuwa na apps muhimu kwa urahisi.
Inasemakana aina ya apps hizo maarufu zitategemea na simu inauzwa kwenda nchi au eneo gani. Mfano simu itakayoletwa Tanzania inaweza kutofautiana na orodha ya apps zinazopatikana kwenye simu kama hiyo hiyo itakayouzwa Urusi. Kwa kifupi ni kwamba watachagua apps hizo 70 maarufu kwa nchi au eneo husika.
Je hii ina maana zitakuja na apps kama WhatsApp, Facebook, Instagram n.k?
Hapana. Apps ambazo zinamilikiwa na makampuni makubwa ya Marekani zitakosekana bado.
Vyanzo: GSMarena na tovuti mbalimbali