Mwaka huu inawezekana tusione toleo kutoka familia ya herufi “G” kwa simu za LG kwa sababu ya muundo wa simu zao zijazo kukubaliwa na mamlaka hivyo basi tutegemee kuziona LG Velvet sokoni.
Kwa wapenzi wa rununu za LG watafurahi kwa kufahamu kuwa kuna simu janja mpya zipo jikoni ambazo zimeshapata kibali kutoka mamlaka husika huko Korea Kusini na tayari zimeshaonekana ingawa ni kwa uchache sana. Hata hivyo, simu hii inafanana kidogo na LG V60 kwa maeneo fulani fulani yanayoifanya iwe ya kuvutia kwa kuangalia kwa mara ya kwanza tu.
Kwa mujibu wa kionjo cha picha mnato kilichowekwa Youtube kwenye chaneli ya Youtube kwanza kabisa inabainisha kuwa simu hiyo itatumia Snapdragon 765G ambacho ni kipuri mama, kamera tatu (3) za nyuma na nyingine mbele. Vilevile, vitufe vitatu kwa ajili ya kuongeza/kupunguza sauti na kingine mahususi kwa kuzima/kuwasha rununu.
Pia, itakuwa na sehemu ya kuchomekea spika za masikioni vilevile zitapatikana katika rangi nne (4) tofauti. Yapo mengi ambayo bado hayajafahamika kuhusu simu hii nikusihi tuu uendelee kutufuatilia kila leo na tutaendelea kuwaletea taarifa kuhusiana na bidhaa hii ya kiganjani.
Vyanzo: GSMArena, The Verge