Shirika la Nokia (Nokia Corporation) la nchini Finland ni moja ya mashirika kongwe duniani katika sekta ya mawasiliano.
Unaweza kuwafahamu zaidi enzi zao za kutuletea simu za Nokia ila tambua shirika hilo lina biashara nyingi zaidi kwenye sekta ya mawasiliano zaidi ya utengenezaji simu kwa sasa. Na simu zao kwa sasa zinatengenezwa kwa lesini na kampuni ya HMD Global.
Baada ya kushindwa biashara ya utengenezaji na uuzaji simu kampuni hiyo ilijidhatiti katika teknolojia na biashara ya huduma za minara.
Taarifa zilizoripotiwa zinasema uongozi wa Nokia unapambana kuepuka kununuliwa kilazima na shirika la uwekezaji ambalo bado halijawekwa wazi.
Nokia kwa sasa wajituma zaidi katika utengenezaji wa teknolojia za kimawasiliano za 5G ili kuwa na uwezo wa kuleta ushindani dhidi ya makampuni kama Huawei na Ericsson, makampuni ambayo kwa kiasi fulani yapo mbele zaidi yao.
Uongozi wa Nokia umeingia makubaliano na benki ya kibiashara ya Citi Group, ambapo benki hiyo kutumia uzoefu wake wa kuwezesha biashara utafanya tathmini ya thamani halisi ya shirika la Nokia kwa sasa. Lengo la uongozi likiwa kuonesha ya kwamba shirika hilo lina utajiri mkubwa kuliko anayetaka kulinunua anataka kulipa, na hivyo kuua mpango wa shirika la uwekezaji kuweza kuwa na uwezo wa kifedha wa kulinunua.
Baada ya kipindi kirefu cha hisa zake kufanya vibaya sokoni tayari hisa zake zimeanza kupanda tangu habari hii ianze kuvuja, wawekezaji wakitegemea kupata faida iwapo shirika linalotaka kuinunua Nokia kama litafanikiwa – kwani wenye hisa nao watalipwa kwenye pesa za manunuzi hayo.
Kuna mengi yameanza kusikika kuhusu walionyuma na ununuzi huu, huku wengine wakisema inawezekana ikawa ni kampuni nyingine kubwa kama vile Samsung. Hii ikiwa ni njia ya kujidhatiti dhidi ya ushindani wa Huawei ambaye yupo vizuri kwenye sekta zote mbili – sekta ya vifaa vya mawasiliano na kwenye bidhaa za kawaida za elektroniki kama vile simu.