Serikali ya Marekani itaweka kampuni nane za China ikiwa ni pamoja na mtengenezaji wa ndege zisizo na rubani DJI kwenye orodha ya kampuni zilizozuiliwa kufanyiwa uwekezaji kwa madai ya kuhusika katika ufuatiliaji wa Waislamu wa Uyghur, gazeti la Financial Times limeripoti.
Makampuni hayo yataripotiwa kuwekwa kwenye orodha ya Idara ya Hazina ya “kampuni tata za kijeshi za viwanda vya China” siku ya Jumanne, kumaanisha kuwa raia wa Marekani watazuiwa kufanya uwekezaji wowote.
Tayari DJI iko kwenye orodha ya Taasisi ya Idara ya Biashara kumaanisha kwamba kampuni za Marekani hazitaweza kuiuza mpaka ziwe na leseni. Wakati huo serikali ilisema ni miongoni mwa makampuni ambayo “yaliwezesha ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu ndani ya Uchina kupitia ukusanyaji na uchambuzi mbaya wa vinasaba au ufuatiliaji wa teknolojia ya juu.” Tofauti na bidhaa za Huawei ndege zisizo na rubani za DJI hazijapigwa marufuku kuuzwa nchini Marekani.
Hatua za hivi punde ni sehemu ya juhudi za Rais wa Marekani Joe Biden kuiwekea vikwazo China kwa ukandamizaji wa Uyghurs na makabila mengine madogo katika eneo la Xinjiang. Wengine ambao wataongezwa kwenye orodha hiyo ni pamoja na kampuni za “Cloud Computing” na kampuni za utambuzi wa uso zinazofanya kazi huko Xinjiang.
Xiaomi iliwekwa kwenye orodha hiyo hiyo ya vizuizi vya uwekezaji mapema mwaka huu. Hata hivyo ilipigana na uamuzi huo ikisema kwamba hakuna mtendaji wake anayejihusisha na jeshi la China na kwamba ukosefu wa uwekezaji wa Marekani ungesababisha “madhara ya haraka na yasiyoweza kurekebishwa.” Mwezi Mei serikali ilikubali kuondoa vikwazo hivyo.
Chanzo: Engadget, Techcrunch na vyanzo vingine.
No Comment! Be the first one.