Apple watengeneza trilioni 3.2 kati ya kupindi cha Krismasi na mwaka mpya 2020. Hayo ni makadirio kwa shillingi za kitanzania baada ya Apple kutangaza mapato ya dola bilioni 1.4 za Kimarekani katika kipindi hicho.
Mapato haya ni asilimia 16 juu ukilinganisha na mapato yaliyopatikana kwenye soko hilo la apps katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2018.
Soko la App Store – ni soko la apps kwa simu zinazotumia programu endeshaji ya iOS na Mac OS.
Wakati mauzo ya simu mpya hayajawa mazuri kwa kipindi cha miaka kadhaa ila inaonekana mauzo ya apps yamekuwa yanapanda kwa kasi sana na hii ni habari nzuri kwa Apple.
Hadi sasa kuna iPhone zinazotumiaka milioni 925 – yaani hizi zinatumika na zimeunganishwa na intaneti.
Watumiaji hawa wa simu wengi wao ni watumiaji wazuri wa apps mbalimbali – ambazo nyingi zake ni za kununua.
Rekodi nyingine iliyofikiwa na Apple ni pamoja na kupata mapato makubwa zaidi kwa siku moja – hii ilifikiwa mwaka mpya – 1/01/2020. Soko la App Store liliingiza dola milioni 386 ndani ya siku moja, hii ikiwa ni juu kwa asilimia 20 ukilinganisha na mapato ya mwaka mpya uliopita. Kumbuka hii ni takribani Tsh Bilioni 887.7.
Kumbuka mauzo ya apps yanapanda sana kipindi hicho cha sikuu kwa sababu kuna kuwa na punguzo kubwa la bei za apps kutoka kwa makampuni mbalimbali. Hili linafanya watu wengi kufanya maamuzi ya manunuzi ya apps nyingi.
Habari hii imesababisha kupanda kwa bei za hisa ya kampuni hiyo kwa takribani asilimia 2.4 kufikia Jumatano.
Tokea kuanzishwa kwake watengenezaji apps wameshalipwa zaidi ya dola bilioni 155 kupitia App Store. Apple kawaida huchukua asilimia 30 ya malipo mauzo ya apps kwenye soko lake la apps.
Soma kuhusu Apps mbalimbali – > Teknokona/Apps