Shirika la Airbus limetangaza kwamba ifikapo mwaka 2021 litasitisha uzalishaji wa ndege zake aina ya A380 superjumbo kutokana na kukosekana kwa soko.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na shirika hilo ifikapo mwaka 2021 oda zilizokuwepo za ndege aina ya A380 zitakabidhiwa kwa wanunuzi na uzalishaji wa ndege hizo utasimamishwa.
Katika taarifa hiyo mkurugenzi mkuu wa Airbus Tom Enders alisema, wametoa tangazo hilo huku wao na wanahisa wengine wanaohusika katika utengenezaji wakiwa na huzuni.
Uamuzi huo umefikiwa baada ya shirika la ndege la Emirates, kutangaza kuwa litapunguza idadi ya ndege za A380 inazohitaji kununua kutoka 162 mpaka 123. Shirika la Emirates ndiyo mteja mkubwa zaidi wa A380 duniani.
Emirates imeingia mkataba mpya wa kununua ndege 70 aina ya A330-900s na a350-900s mbadala wa A380. Mkataba huo mpya una thamani ya dola bilioni 21.4.
Ndege hizi zenye uwezo wa kubeba zaidi ya abiria 850 zilizalishwa kutoa ushindani kwa ndege aina ya Boeing 747 za shirika la uzalishaji ndege la Marekani. Ndege hiyo iliyogharimu mabilioni ya dola kuibuni na kuiunda, imeshindwa kupata wateja wengi katika soko ambalo hivi sasa linaegemea zaidi katika ndege zenye ukubwa wa kati. Ila bado Airbus hawajapata hasara.
Boeing ya Marekani ambayo ni mpinzani wa Airbus, ilisita kuunda ndege kubwa kama A380, badala yake ilielekeza nguvu kuunda 787 Dreamliner ambayo inatumia mafuta vizuri na ukubwa wake unafaa kutumika katika viwanja vingi kwa urahisi.