Wakati mauzo ya simu za makampuni ya China yanaonekana kuweza kuathirika na siasa nchini Marekani hali ni tofauti katika bara la Ulaya. Data za mauzo ya simu zinaonesha mauzo ya simu hizo yanazidi kukua barani Ulaya.
Data kutoka shirika la utafiti wa masoko la Canalys linaonesha kwa mwaka 2018 kulikuwa na ukuaji mkubwa wa soko la simu kutoka makampuni ya China barani Ulaya.
Makampuni yaliyofanya vizuri ni pamoja na Huawei, Xiaomi, Oppo na OnePlus. Asilimia 32 ya mauzo ya simu barani humo yalikuwa kutoka makampuni ya simu ya kutoka China.
Huawei alifikisha asilimia 23 ya soko zima wakati Xiaomi alikua kutoka asilimia 3.6 mwaka 2017 na hadi kufikia asilimia 6 mwishoni mwa mwaka 2018.
Hali ya kisiasi nchini Marekani dhidi ya makampuni ya mawasiliano ya nchini China ni mbaya kwa sasa. Tayari makampuni kama ZTE na Huawei yameathirika kimauzo kutokana na uamuzi wa watengenezaji sera za kiusalama nchini humo kuyaweka katika orodha ya makampuni ambazo bidhaa zake kama simu na vifaa vya mawasiliano/simu haziaminiwi – wakiamini kuna jinsi wanashirikiana na serikali ya China kudukua data.
Hali hii ya Marekani imezifanya kampuni nyingi za China kuzidi kuwekeza kimauzo katika masoko mengine kama bara la Ulaya. Uwekezaji huu unaonesha unafanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani tayari simu za nchini China zimeanza kuwa zina ubora wa hali ya juu wa kuweza kushindana na simu kutoka Korea na za makampuni ya Ulaya.
Data za kimauzo za Canalys zinaonesha Apple iliingiza simu milioni 42.8 kufikia mwisho wa mwaka 2018 barani Ulaya, kipindi hicho hicho Huawei aliingiza simu milioni 42.5. Inakisiwa kufikiwa mwisho wa mwaka basi Huawei itaipita kampuni ya Apple barani Ulaya na kushikilia nafasi ya pili kwenye soko, nyuma ya Samsung.