Je neno ukuta wa Urusi linaweza kuwa sawa kwa kinachoweza tokea nchini Urusi? Duma – bunge dogo la nchini Urusi limepitisha mswada ambao unalenga kuifanya huduma ya intaneti ya nchi kuwa huru zaidi kutoka kwenye intaneti ya kimataifa.
Kabla ya kuendelea vizuri ni bora kuelewa kwa undani intaneti ni nini.
Kwa maneno marahisi, nini maana ya intaneti?
Intaneti ni huduma ya muunganisho wa kompyuta mbalimbali duniani unaoruhusu mtu mwenye haki ya taarifa flani iliyo kwenye kompyuta nyingine (bila kujali mipaka ya miji, nchi, au bara). Kompyuta hizi zinaweza kuwasiliana kwa mfumo wa waya, na usio wa waya (wifi au faiba).
Muswada huu ukifika bunge la juu na kisha kupitishwa na rais basi intaneti ya Urusi itakuwa huru sana nje ya mfumo mzima wa intaneti wa dunia.
Kwa maelezo madogo ya nini maana ya mfumo wa intaneti hapo juu utakuwa umedungua ya kwamba huwa intaneti inakuonganisha moja kwa moja na ile kompyuta yenye data (hapa ni tovuti/website) unayohitaji. Mfumo ambao mswada huu utatengeneza utamaanisha lazima utakapobofya kutembelea tovuti flani basi kompyuta yako haitaunganishwa moja kwa moja na server(kompyuta) yenye data husika, bali utaunganishwa kupitia mfumo spesheli wa usimamizi wa intaneti kati ya Urusi na intaneti kuu ya dunia.
Hii imefananishwa na intaneti ya China, ambayo pia inapitia mfumo kama huu. Intaneti ya mfumo huu inafanya huduma za intaneti za ndani zikue zaidi na pia mashirika ya usimamizi wa huduma ya intaneti wanaweza kuzuia tovuti kupatikana kwenye nchi kwa urahisi zaidi – kwani huduma ya intaneti kati ya nchi na mataifa mengine hupitia kwenye vifaa spesheli vinavyoweza kusimamiwa na serikali.
Intaneti ya dunia ipo huru sana. Huduma ya intaneti ni ya moja kwa moja bila usimamizi unaobana kuhusu data zinazopita.
Inategemewa ikifikia hatua ya kuwa sheria watoa huduma wa intaneti watatakiwa kutumia vifaa vipya vya network vitakavyowezesha usimamizi wa juu wa data kati ya mtoa huduma na mteja dhidi ya intaneti kuu – yaani ya dunia. Muswada utafikishwa bunge la juu la nchi hiyo tarehe 22 Aprili.
Wanaotetea mswada huu wanasema hii ni kuisaidia Urusi kuwa huru zaidi kwenye huduma ya intaneti ili kujilinda dhidi ya vikwazo vinavyoweza kuwekwa dhidi yake na mataifa ya magharibi. Wengine wanapinga wakisema taifa la Urusi linataka kubana na kufuatilia utumiaji wa intaneti wa wananchi wake kufanana na mfumo wa intaneti wa Uchina ambao umepiwa jina la utani la Great Wall of China (ukuta mkuu wa China).