Jumamosi imeweka rekodi kubwa katika sekta ya safari za anga za juu. Nasa na SpaceX walifanikisha safari ya kwanza ya wanasayansi kwenda anga za juu kupitia ushirikiano wao.
Hii ni mara ya kwanza kwa kifaa kilichotengenezwa na kumilikiwa na kampuni binafsi kupeleka wanasayansi katika kituo cha kimataifa cha angani (International Space Station).
SpaceX ni kampuni iliyoanzishwa na Elon Musk mwaka 2002 ikiwa na lengo la kushusha gharama za safari za anga na pia kuwezesha safari za kwenda kwenye sayari ya Mirihi / Masi. Hii ndio kampuni ya kwanza binafsi kupeleka mizigo kwenye kituo cha anga cha kimataifa na pia kwa sasa imekuwa ndiyo ya kwanza kupeleka wanasayansi kwenye kituo hicho pia.
Kwa nini SpaceX wametumika?
Ni zaidi ya miaka nane sasa tokea NASA (Shirika la Serikali ya Marekani linalohusika na utafiti wa anga) kupeleka watafiti/wanasayansi wake kwenye kituo hicho cha anga kwa kutumia chombo chake chenyewe. Kwa muda mrefu wamekuwa wakiwategemea Urusi kwenye usafirishaji wa wanasayansi wao kwenda kwenye kituo hicho cha anga, na wamekuwa wakiwalipa pesa nyingi.
SpaceX wamekuja na teknolojia inayowaruhusu kutumika tena kwa vifaa vyao vya usafirishaji (roketi). Kutokana na teknolojia hiyo wameweza kushusha sana gharama za uendeshaji. Teknolojia ya rokoti inayotumiwa na Urusi na ata NASA inahusisha kutoweza kutumika tena kwa rokoti baada ya kuruka – huwa zinachomoka zikifika anga za juu na hivyo kuharibika / kuungua baada ya utumiaji.
Kupitia ushirikiano huu na SpaceX, NASA wanategemea kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za safari zake na pia ni jambo la sifa kwa taifa la Marekani kwa kutokuwa tegemezi kwa huduma za Urusi.
Gharama za safari kwa kuwatumia SpaceX ni takribani robo ya gharama ya safari hiyo hiyo kwa kutumia mashirika mengine ya anga.