Kampuni ya simu yenye makao makuu yake Uchina, Xiaomi imetangaza kufungua maduka ya uuzaji wa simu zake Mi Store yapatayo zaidi ya 500 kwa wakati (siku) mmoja nchini India katika majimbo 14.
Takwimu hii ni nzuri kwa Xiaomi na imeifanya kuingia kwenye kitabu maarufu cha rekodi za matukio duniani cha Guinness (Guinness World Record). Xiaomi imepata kuingia kwenye kitabu hicho kwa kuzindua sehemu nyingi za kuuza simu/bidhaa zake kwa wakati mmoja.
Haishangazi Xiaomi kuwa na sehemu nyingi za kuchuuza kwani hata iPhone ina maduka 198 nchini Marekani pekee japo hayakufunguliwa kwa wakati mmoja.
Kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa Xiaomi nchini India, aliweka wazi kuwa mpango wao ni kufungua maduka zaidi ya 5000 ambayo yatatoa ajira 15,000 itakapofika mwishoni mwa mwaka 2019.
Lengo la Xiaomi ni kupeleka simu zao mpaka maeneo ya vijijini ambako bidhaa zake bado hazijafika. Xiaomi wamelazimika kufungua maduka mengi yasiyo ya kimtandao (offline) ili kuwafikia moja kwa moja wananchi walio wengi ambao hawakuwahi kuona simu zao.