Ni dhahiri kuwa watu wengi hutumia Facebook hata wanapokuwa makazini – wengi kiwizi wizi. Faceboook wamekuja na Facebook ambayo ni mahususi kwa ajili ya mambo yanayohusiana na ofisi tu.
Mpango huo ulioitwa WorkPlace utakuwa ni kwa ajili ya mawasiliano kupitia Facebook ambapo ni maalum kwa ajili masuala ya ofisi.
Facebook at Work, ambayo sasa inafahamika kwa jina la WorkPlace, haitachanganya ujumbe, makundi au vitu unavyoandika kwenye mtandao wa kawaida wa Facebook kwa ajili ya wengine kusoma na akaunti yako binafsi (ile unayoitumia siku zote).
Huduma ya Workplace itaweza kutumika kwenye simu janja zenye kutumia Android au iOS na kupitia tovuti spesheli kwenye kompyuta.
Jambo hili si geni sana kwa wale tunafuatilia masuala ya teknolojia kama TeknoKona kwani mwaka 2014 Facebook walisema kuwa wana mpango wa kuja na Facebook kwa ajili ya maofisi/makampuni mbalimbali.
Kupitia huduma hii makampuni hata yale makubwa sana yataweza kupunguza kwa kiasi kikubwa utumiaji wa huduma za barua pepe kwa mazungumzo madogo madogo na hata yale makubwa sana.
Na wiki hii wamefanikiwa kutimiza mpango wao na wameshirikisha makampuni makubwa kama Google na Microsoft kuweza kufikisha mpango huo mbali zaidi na kwa hakika mapato ya Facebook huenda yakaongezeka mara dufu.
Kwa sasa mtandao huo tayari upo hewani lakini bado upo katika hatua ya majaribio. Kampuni yoyote inaweza kuomba kuanza kutumia huduma hiyo mara moja. TeknoKona tutawajulisha pale itakapokuwa ikipatikana duniani kote.
Tovuti ya Facebook at Work (Workplace) – https://workplace.fb.com/
Vyanzo: the guardian, pamoja na mitandao mbalimbali.