WhatsApp inafanya maboresho makubwa ya kimuundo tangu kuanzishwa kwake miaka takribani nane iliyopita, kuanzia sasa watumiaji wa mtandao huo sasa wataweza kuweka status ambazo zinajifuta baada ya masaa 24.
Maboresho haya yanategemewa kusambazwa kwa watumiaji ulimwengu mzima kwa taratibu kuanzia tarehe 20/02/2017, katika hali ya kawaida tunategemea ndani ya mwezi mmoja ujao watumiaji wengi watakuwa tayari wamepata toleo jipya. Kama toleo hilo jipya la WhatsApp limekufikia katika soko la apps katika simu yako basi unachohitaji ni kusanikisha na kisha utaweza kuenjoy huduma hiyo.
Je toleo hili linakuja na nini kipya?!
Kwa ufupi toleo jipya la WhatsApp litaleta kipengere kipya ambacho watumiaji wataweza kusambaza video, picha, au GIF.
Kama unahisi kitu hiki sio kipya ni kweli sio kipya maana hii ndio namna ambayo mtandao wa Snapchat umekuwa ukifanya kazi, tayari Instagram walikwishaiga mtindo huu wa ‘stories’ hivyo WhatsApp ni kampuni ya pili inayomilikiwa na Facebook kuiga mtindo huu.
Je maboresho haya yana maana gani hasa?!
Kibiashara kampuni ya WhatsApp tofauti na Facebook na Instagram bado haija fungua milango yake kwa matangazo. Hivi karibuni vyanzo viliwanukuu wamiliki wa mtandao huo wakisema kwamba wanatafuta namna ambayo wataweza kuleta matangazo katika app hii, wengi wanaamini maboresho haya yanalenga kuleta matangazo katika app hii pendwa.
Ikumbukwe kwamba mitandao kama Twitter tayari ipo katika matatizo kutokana na kushindwa kutengeneza mapato ya kutosha, maboresho haya ni wazi yanalenga katika kuifanya app hii kutengeneza pesa zaidi.