Zoezi la WhatsApp kuwafungia kwa muda watumiaji wa GB WhatsApp na WhatsApp Plus lilianza takribani miezi miwili iliyopita limezidi kuchachamaa, na sasa kampuni ya WhatsApp imetoa angalizo kwa wale ambao hurudi tena kwenye apps hizo tena na tena.
Katika taarifa rasmi iliyotolewa na WhatsApp – inayomilikiwa na kampuni ya Facebook, wamesema “kama unapokea ujumbe ndani ya app ikisema akaunti yako imefungiwa kwa muda (temporarily banned) ina maanisha unatumia toleo lisilo rasmi la WhatsApp.
Kama hautobadili na kuanza kutumia toleo rasmi la WhatsApp baada ya muda ya kufungiwa, akaunti yako ipo katika hatari ya kufungiwa mazima kwenye huduma ya WhatsApp.”
Tayari Facebook wameonesha wapo njiani kukaribisha matangazo kwenye app ya WhatsApp na hivyo uwepo wa matoleo ya WhatsApp ambayo si rasmi ni hatari katika mpango wao huo. Ila pia ni matoleo ambayo data za mtumiaji zipo kwenye hatari ya udukuzi.
Je upo tayari kuhamia toleo rasmi? Basi fuata njia hizi kuhakikisha haupotezi data zako za mazungumzo
Kama ulikuwa unatumia GB WhatsApp:
- Subiria muda wa kufungiwa kupitia (temporary ban)
- Kisha ingia kwenye GB WhatsApp na kisha nenda – More Options -> Chats -> Backup Chats
- Kisha nenda kwenye app ya Files na kisha tafuta faili la GB WhatsApp, ukilipata libadili jina (rename) kutoka GB WhatsApp kwenda jina la WhatsApp
- Nenda Google PlayStore na shusha app ya WhatsApp, fungua na hakiki namba
- Itakapokuletea suala la Backup, bofya Restore -> Next
- App ya WhatsApp itatumia data za chati za GB WhatsApp na sasa utaweza kuiondoa GB WhatsApp.
Kwa watumiaji wa WhatsApp Plus hali ni tofauti kwani hauitaji kuchukua hatua nyingi. Hakikisha umefanya backup, kisha install app ya WhatsApp. App ya WhatsApp itaweza kurudisha data za WhatsApp Plus moja kwa moja kwenye hatua ya kurestore.
Tunakushauri kama umekuwa mtumiaji wa WhatsApp Plus na GB WhatsApp kama namba unayotumia ni muhimu kwako kwa mawasiliano ni bora uhamie kwenye WhatsApp rasmi.