Nchini Uingereza watu kadhaa wachoma moto minara ya 5G na vifaa vyake kutokana na kuamini habari za uongo kwamba teknolojia hiyo inasambaza virusi vya Corona.
Ni jambo ambalo huwezi kulifikiria kutokea katika nchi zilizoendelea lakini jambo linaloonesha kwa kiasi gani habari za uongo (fake news) zinaweza kuleta hasara kubwa katika jamii.
Hivi karibuni kuna uvumi ulisambazwa sana mtandaoni ukihusisha teknolojia ya 5G ambayo ilianza kutumika zaidi nchini China kama sababu moja kuu ya ujio wa ugonjwa wa Corona.
Watu ambao wameamini taarifa hiyo potovu ya kutengenezwa wamesababisha hasara kwa makampuni kadhaa nchini Uingereza ambayo yalishaanza usambazaji wa huduma za teknolojia hiyo ya kisasa zaidi katika huduma ya intaneti.
Katika kipindi cha wiki moja iliyopita zaidi ya minara mitatu ya 5G inayomilikiwa na Vodafone uingereza iliharibiwa kwa moto. Na huko jijini Birmingham mnara ambao hata ulikuwa hautoi huduma ya 5G bali ni 2G,3G na 4G unaomilikiwa na kampuni nyingine ya EE nao ulichomwa moja.
Video ikionesha wafanyakazi wanaosambaza nyaya za huduma ya 5G wakisumbuliwa na mtu anayeamini 5G inahusika kwenye usambazaji wa virusi vya Corona.
This is the consequence of those bonkers Facebook conspiracy theories about 5G. Key workers getting harassed on the street. pic.twitter.com/5z35r6sabp
— Charlie Haynes (@charliehtweets) April 2, 2020
Hatua Zachukuliwa:
> Imeripotiwa mtandao wa YouTube tayari unachukulia hatua video zozote zinazowekwa kwenye mtandao huo zinazosambaza uzushi wa aina yeyote unaohusisha teknolojia ya 5G na gonjwa la korona.
> Pia kuna chombo cha habari, redio ya ngazi ya jamii, inachukuliwa hatua kwa kumualika mhudumu wa afya, nesi, aliyeongea kwenye kipindi akidai teknolojia ya 5G inanyonya gesi ya oksijeni kutoka kwenye mapafu ya watu.
Uvumi usio wa kweli umesambaa kwa haraka zaidi na sasa ndio watu wameamka na kuamua kuchukua hatua baada ya kuona hasara na hatari inayoanza kujitokeza. Uelewa mdogo wa teknolojia ya 5G unaonekana kuchangia katika upotoshwaji huo.