Familia ya simu janja ambazo zinaweza zikakunjika na kukunjuka kutoka Samsung zinaendelea kuongezeka ambapo wanafamilia wapya kwa maana ya Galaxy Z Flip4 na Z Fold4 zitazinduliwa mnamo Agosti 10 ya mwaka huu.
Huu ni mwendelezo wa kile ambacho Samsung iliamua kuzirudisha kwenye ulingo simu ambazo zina muundo wa kukunjika na kukunjuka na dunia nzima inafahamu kuhusu Z Flip3 na Z Fold3 ambazo ndio toleo la sasa lakini ni suala la siku kadhaa zijazo ambapo dunia itapata kufahamu yote yanayohusu toleo jipya la rununu kutoka kwenye familia ya Z Fold na Z Flip.
Uzinduzi huo ambao utakuwa mubashara kupitia YouTube na chaneli ya Samsung utaanza saa 10 jioni (saa za Afrika Mashariki), Agosti 10 2022 amabapo mbali na Samsung Galaxy Z Fold4 na Z Flip4 pia Galaxy watch5 na toleo jipya la Galaxy Buds vitazinduliwa.
Zimekuwepo habari za chini kwa chini (fununu) kuhusu sifa ambazo simu janja hizo zinazo kuanzia kwenyw muonekano wake hadi kwenye bei ikiwa ni katika kuleta utofauti wa toleo lililopo sokoni hivi sasa na hilo ambalo litazinduliwa Agosti 10 lakini ukweli ni kwamba ulimwengu utafahamu kinagaubaga undani wa bidhaa hizo za kidijitali kwa urahisi kabisa bila gharama yoyote ile.
TeknoKona kama mdau wa masuala ya teknolojia tutawaletea undani wa uzinduzi huo mara baada ya kila kitu kuwa wazi (rasmi). Tukusihi uendelee kutufuatilia kwa habari mbalimbali za ndani na nje ya Tanzania zinazohusu teknolojia.
Vyanzo: GSMArena, mitanadao mbalimbali
One Comment