Wakati kampuni ya Google jumatatu inatarajia kuzindua toleo jipya la Mfumo endeshi wa Simu janja wa Android tayari makisio ya wengi ya jina la toleo hilo yametolewa.
Toleo hilo kwa sasa linaitwa Android O kwa sababu jina litakuwa linaanzia na herufi O kwa mpangilio waliouweka wenyewe Google. Jina linalotarajiwa na wengi zaidi kupewa toleo hilo ni Oreo.
Wengi wameweka dhana hiyo baada ya kuvuja kwa faili la video lililoonekana na mtu aliyedai ameona jina la Oreo. Oreo ni aina ya Chokoleti tamu ambazo ni maarufu sana nchini Marekani
Hata hivyo inasemekana baada ya muda mfupi Faili hilo lilibadilishwa jina na kuwekwa Octopus (Pweza). Hata hivyo bado hakuna uhakika wa jina gani toleo hilo litabeba.
Google imekuwa ikiyapa majina ya Pipi au Chokoleti matoleo yake ya Android kwa kufuatisha mpangilio sawia wa herufi.
Wengi hawataraji jina la toleo jipya kuwa Octopus kwani itakuwa ni kinyume na utaratibu wa utoaji wa majina ya matoleo ya Android, ambapo hutoa kwa kwa pipi na Chokoleti na si kwa vyakula vya baharini.
Mbali na jina hilo la Oreo, majina mengine yanayotarajiwa pengine yanaweza kubeba jina toleo hilo la nane la Android ni Oatmeal, Orellete, Oatcake, OH Henry, Octopus, Olives, Omega spread, Oca, Ocean Perch, Oat milk nk.
Toleo hilo jipya linatarajiwa kuwa na maboresho mengi mazuri ikiwemo ulaji mdogo wa chaji ya betri, Fonts mpya za kupakuwa na mengi mengi.
Endelea kutembelea Teknokona kwa kujua jina la toleo jipya la Android O na mengine mengi.