Biashara katika makundi ya mtandao wa kijamii wa Facebook imeonesha kukua na kutishia kuzidi maduka maalum ya mtandaoni yanayouza bidhaa zake kupitia mfumo wa kutumia wavuti.
Kwa mujibu wa ripoti ya utafiti iliyotolewa na Geopoll inaonesha mtandao wa Facebook ni wa pili katika mauzo ya kimtandao kwa asilimia 32 baada ya Jumia inayoongoza katika soko hilo kwa asilimia 56.
Utafiti huu umefanywa kwa nchi za Kenya, Nigeria na Afrika Kusini na kati ya watu 2,031 waliohojiwa kutoka Kenya, Nigeria na Afrika Kusini, Jumia imeongoza kwa umaarufu miongoni mwa wanunuaji wa bidhaa kwa njia ya mtandao. Facebook ni tishio katika soko la kidijitali, ripoti ya utafiti huo ilionyesha.
Kati ya waliohojiwa, asilimia 74 walisema kwa wakati mmoja walinunua bidhaa kupitia mtandaoni, ishara kwamba watu wameanza kuzoea kununua bidhaa katika soko hilo.