Mfumo endeshi (Operating System) wa Android kwa mara ya kwanza umeongoza kama mfumo unaotumiwa na watu wengi zaidi duniani kwa sasa.
Kwa mujibu wa ripoti ya kampuni ya StatCounter uliotolewa mwezi huu, inasema kwamba watumiaji wa Mfumo endeshi wa Android ndio wanaoongoza kwa sasa mbele ya mfumo wa Windows katika kutembelea kurasa mbalimbali za mitandao.
Utafiti huo uliofanyika kwa mwezi mmoja umetumia Tovuti milioni 2.5 ambapo zinawatumiaji bilioni 15. Mifumo endeshi iliyohusishwa katika utafiti huo ni Android, Windows, iOS, OS X(MacOS) na Linux.
Vifaa vilivyofanyiwa utafiti katika kuperuzi kurasa za Intaneti ni Kompyuta za mezani(Desktop), Kompyuta mpakato(Laptop), Tablet na  mkusanyiko wa Simu Janja.
Ripoti imebainisha Kwa sasa watumiaji wa Android ni asilimia 37.93 na wale wa Windows ni asilimia 37.91. Mfumo wa iOS unafuatia kwa kuwa na watumiaji asilimia 13.09 na Mfumo wa OS X(MacOS) asilimia 5.17 na Mfumo wa Linux asilimia 0.75.
Maeneo ya Asia watumiaji wa Android ni asilimia 52.2% kulinganisha na asilimia 29.2% ya watumiaji wa Windows. Ulaya asilimia 51.7% wanatumia Windows na asilimia 23.6% ni watumiaji wa Android. Hata hivyo kwa mujibu wa ripoti hiyo bado inaonesha soko la Windows lipo juu kwa asilimia 84.
Aidha ripoti hiyo imebainisha kuongezeka zaidi kwa watu kutumia simu za mkononi zaidi kuliko Kompyuta katika matumizi mbalimbali hususani ya Intaneti.
Utafiti huu ni kwa ajili ya matumizi ya Intaneti, ndio umebaini kwamba mfumo wa Android unatumika zaidi kuliko mfumo mwingine. Windows bado wanaendelea kutawala soko la Kompyuta na huku Android ikiendelea kuongoza soko la Simu Janja.
Mkurugenzi Mtendaji wa StatCounter, bwana Aodhan Cullen alisema, matokeo hayo ni alama ya mwisho ya uongozi wa OS ya Microsoft katika soko duniani kote ambayo imekuwa ikiongoza tangu miaka ya 1980.
Pia aliongeza kusema ni mafanikio makubwa kwa Android ambayo imeweza kuwa na watumiaji wengi kwa muda wa miaka mitano iliyopita.